Waziri wa Uhamiaji wa Uingereza, Robert Jenrick amejiuzulu baada ya serikali ya nchi hiyo kuchapisha sheria kuhusu mkataba wenye utata na Rwanda wa kutuma wahamiaji katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Waziri wa Mambo ya Ndani, James Cleverly aliwaambia wabunge jana Jumatano kwamba Robert Jenrick amejiuzulu kwa madai kuwa sheria hiyo ya dharura haijitoshelezi.
“ Sikubaliani na sheria inayopendekezwa kwa sasa kupitia Bunge, kwani siamini kwamba inatupa fursa nzuri zaidi ya kufanikiwa,” ameandika waziri huyo katika barua aliyoielekeza kwa Waziri Mkuu wa Uingereza, Rishi Sunak.
Mapema Jumatano Rwanda ilionya kujiondoa katika mkataba wa kuwapokea wahamiaji iwapo Uingereza haitaheshimu sheria za kimataifa.
Uingereza na Rwanda zilitia saini mkataba mpya Jumanne katika jitihada za kufufua pendekezo linaloonekana kuwa na utata la Uingereza la kuwahamisha wahamiaji katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki, pendekezo ambalo awali lilipingwa na mahakama ya Uingereza.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Vincent Biruta, ambaye alitia saini mkataba huo wa pande mbili, alisema ukiukaji wowote wa mikataba ya kimataifa unaweza kuifanya Rwanda kujiondoa katika mkataba huo.
Mpango wa Rwanda ni sehemu ya mkakati wa kupunguza idadi ya watu wanaoingia nchini Uingereza kwa kuvuka bahari kwa boti.
Leave a comment