RIPOTI ya Haki za Binadamu Tanzania ya 2021, iliyoandaliwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), imebaini uwepo wa matukio ya watu kuchukuliwa na watu wasiojulikana. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo, leo Jumatatu, tarehe 11 Aprili 2022, jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga amesema kituo chake kilipokea kesi 12 za watu waliopotezwa na watu wasiojulikana.
“Matukio ya kutoweka pia yalizorotesha haki ya uhuru na usalama wa mtu binafsi, katika 2021, LHRC iliweka kumbukumbu ya kesi 12 za watu walioripotiwa kuchukuliwa na watu wasiojulikana na kupotea,” amesema Henga.
Katika hatua nyingine, Henga amesema ripoti ya LHRC imebaini kuongezeka kwa mauaji yanayotokana na wananchi kujichukulia sheria mkononi na imani za kishirikina.
“Mauaji yanayotokana na wananchi kujichukulia sheria mkononi kwa 2021, yaliongezeka kwa 6.8% ikilinganishwa na mwaka wa 2020, wakati mauaji yaliyochochewa na uchawi au imani za kishirikina yaliongezeka kwa 38.4%,” amesema Henga.
Aidha, Henga amesema ripoti yao imebaini kuna mabadiliko katika haki ya uhuru wa kujieleza kwa 2021, ingawa bado kuna matukio saba ya waandishi wa habari kukamatwa kinyume cha sheria.
“Sheria na kanuni bado ni changamoto, hasa zile zenye vikwazo katika ufurahiaji wa haki hii ikiwemo Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya 2016, Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015.
“Na Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta. (Maudhui ya Mtandaoni), Kanuni za mwaka 2020 za mwaka 2021. LHRC iliweka kumbukumbu ya jumla ya matukio saba ya ukamataji usio halali wa waandishi wa habari,” amesema Henga.
Henga amesema, LHRC inaishauri Serikali kuendelea kulinda haki za binadamu.
LHRC inatoa rai serikali na jamii ya Watanzania kuendelea kulinda haki za binadamu na kuwawajibisha wale ambao wameshindwa kuheshimu haki hizo bila ubaguzi wa kikabila, kidini, ki chama na kijinsia ili tuweze kuifikia jamii yenye haki na usawa-Mkurugenzi Mtendaji LHRC, Anna Henga.
Leave a comment