RAIS Daktari Samia Suluhu Hassan, amesema aliyekuwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Paul Makonda, alikiamsha chama hicho kutoka usingizini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, ametoa kauli hiyo leo tarehe 4 Aprili 2024, Ikulu jijini Dar es Salaam, akimuapisha Makonda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, pamoja na viongozi wengine aliowateua hivi karibuni.
“Paul umefanya kazi nzuri CCM, umekichemsha chama, ilikuwa chama kidogo kina… kila mmoja mvivu kutoka hataki, sinzia sinzia lakini umeingia njiani umekichemsha chama tumeamka vizuri sana,” amesema Rais Samia.
Baada ya Makonda aliyekitumikia cheo cha uenezi wa CCM kwa takribani miezi mitano baada ya kuteuliwa Oktoba 2023, kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, chama hicho kimemteua Amos Makala, kurithi mikoba yake.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amemuagiza Makonda akaimarishe mazingira ya utalii jijini Arusha, ikiwemo kushirikiana na wawekezaji katika kutatua changamoto ya malazi kwa watalii.
“Tumekupeleka Arusha unajua nini kipo Arusha na unajua matumaini yangu kwako kwa Arusha. Nenda kafanye kazi Arusha, mimi nina imani kubwa nawe na najua utafanya mimi ninachotaka kufanya. Kubwa Arusha utalii umekuwa mkubwa sana wageni wengi malazi hakuna, nenda ukasimamie ukisaidiana na wawekezaji kuhakikisha tunapata malazi mengi kwa wageni wetu,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Arusha ni mji mkubwa sana, makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki lakini mataasisi makubwa ya kimataifa yapo Arusha, kasimamie mkoa uwe na jina zuri.”
Leave a comment