RAIS Samia Suluhu Hassan, amewaagiza mawaziri wake wakafanyie kazi ripoti ya ukaguzi uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), kwa mwaka wa fedha wa 2022/23, ili hoja zilizoibuliwa zijibiwe kabla haijajadiliwa bungeni jijini Dodoma. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Mkuu huyo wa nchi ametoa agizo hilo leo tarehe 4 Aprili 2024, Ikulu ya jijini Dar es salaam, akiwaapisha viongozi aliowateua hivi karibuni.
“Mengine nataka mkayashughulikie, CAG juzi ametoa ripoti amesema mambo kadhaa yanayowahusu. Hivyo mawaziri wote mliopo kwenye ripoti ya CAG mkayasimamie, mkayafanyie kazi, hoja zijibiwe… Bunge litakapoijadili hoja ziwe zimejibiwa na mkijibu haraka tutapata kujua yepi yamejibika, yepi hayajajibika na hatua gani zichukuliwe, wote mkasimamie hayo,” amesema Rais Samia.
Rais Samia ametoa agizo hilo siku chache baada ya kukabidhiwa ripoti hiyo na CAG Charles Kichere, ambayo baadae ataikabidhi bungeni kwa ajili ya kujadiliwa.
Katika ripoti yake, CAG Kichere alisema hati safi zimeongezeka hadi kufikia asilimia 99 huku hati chafu ikiwa moja.
Hata hivyo, CAG Kichere aliibua madudu katika baadhi ya halmashauri ikiwemo baadhi yake kulipa fedha za miradi bila ya nyaraka.
Ingekuwa Hati safi ni sawa na uadilifu au Uaminifu tungekuwa mbali Sana kiuchumi lkn