RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali yake inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali, kwa ajili ya kumsaidia mkulima kupata masoko ya mazao yake hasa kutoka nje ya nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mkuu huyo wa nchi ametaja mikakati hiyo leo tarehe 7 Septemba 2023, aliposhiriki Jukwaa la Mfumo wa Chakula Afrika, jijini Dar es Salaam.
Miongoni mwa mikakati iliyotajwa na Rais Samia, ni uboreshaji bandari za Tanzania kwa kujenga sehemu maalum za kuhifadhia mazao ili yasiharibike wakati yanasubiri usafiri wa kupelekwa katika masoko nje ya nchi.
“Pale bandarini tunajenga sehemu ambayo itaweza kuhifadhi mazao yanayoharibika kwa haraka, yaweze kuhifadhiwa wakati yanasubiri usafiri. Tunachukua hatua zote ili kufikisha mazao kwenye soko,” amesema Rais Samia.
Mkakati mwingine ni kuendelea kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uongezaji thamani bidhaa za mazao, ili kuwainua wakulima hususan vijana waliounganishwa katika mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT).
Katika hatua nyingine, Rais Samia alisema Serikali yake inaendelea kuimarisha mitandao ya barabara za wilaya na zile zinazounganisha nchi jirani, ili kuhakikisha mazao ya wakulima hayakwami shambani badala yake yanafika kwa wakati sokoni.
Rais Samia amesema, Serikali yake itaendelea kuwanganisha wakulima na masoko moja kwa moja, ili kukwepa madalali ambao wanawanyonya kwa kununua mazao yao kwa bei ndogo.
Kiongozi huyo alitaja mikakati hiyo wakati anaelezea changamoto wanazopitia wakulima, ambapo alizitaja mbili, moja ikiwa ni kutojua mahitaji ya soko na namna ya kuwafikia wateja.
“Kuna shida katika kupatikana masoko lakini katika tafiti tumegundua kuna mambo mawili yana utata na tunayafanyia kazi. La kwanza ni kujua mahitaji ya bidhaa gani inatakiwa na wapi, tukijua hilo tunajua kinachozalishwa upande mmoja kiende upande mwingine. Pili ni muunganiko kati ya wakulima na soko,” amesema Rais Samia.
Leave a comment