RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesaini miswada ya sheria za uchaguzi kwa ajili ya kuwa sheria kamili na kuanza kutumika, licha ya kelele za wapinzani zilizomtaka asisaini ili ifanyiwe marekebisho hayo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 2 Aprili 2024, bungeni jijini Dodoma na Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson.
“Katika mkutano wa 14 wa Bunge, Bunge lilipitisha miswada minne ya sheria na kwa taarifa hii napenda kulitaarifu Bunge kuwa tayari miswada hiyo minne imepata kibali cha Rais Samia na kuwa sheria za nchi, kwa hiyo zimeshakua sheria kamili na Rais ameshafanya kwa sehemu yake,” amesema Spika Tulia.
Muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa 2023 umesainiwa na kuwa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani namba 1 ya 2024. Muswada wa Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi wa 2023 umekuwa Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Namba 2 ya 2024.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Vyama vya Siasa wa 2023, umekuwa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Vyama vya Siasa namba 3 ya 2024 na muswada wa mwisho uliosainiwa umekuwa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali namba 4 ya 2024.
Miswada hiyo imesainiwa katika kipindi ambacho baadhi ya vyama vya siasa vya upinzani hususan Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kikimtaka Rais Samia asiisaini ili ifanyiwe marekebisho kwa madai kuwa ina dosari ambazo hazitatatua changamoto za kiuchaguzi.
Hata hivyo, Serikali imekuwa ikisema miswada hiyo ina lengo la kuhakikisha upatikanaji wa chaguzi huru na za haki.
Leave a comment