JESHI la Polisi visiwani Zanzibar, limesema halijawakamata watu 12 kwa sababu ya kula hadharani wakati wa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani, bali liliwakamata kwa makosa ya matumizi ya dawa za kulevya aina ya bangi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Ufafanuzi huo umetolewa na Kamishna Mkuu wa Jeshi la Polisi Zanzibar, CP Hamad Hamis Hamad, baada ya tukio hilo kuibua mjadala mtandaoni huku baadhi ya watu wakihoji kwa nini wakamatwe kwa kosa la kula hadharani mchana.
CP Hamad alisema watu hao hawajakamatwa kwa sababu ya kula hadharani kwani hakuna sheria inayokataza suala hilo, bali walikamatwa kwa kuwa walikuwa katika maeneo ambayo kulikuwa na watu wengine ambao walikuwa wanavuta bangi hadharani.
“Jeshi la Polisi lilipokea taarifa watu hao walikuwa wanavuta bangi hadharani mchana kinyume cha sheria na watu wengine mchana walikutwa katika tukio hili. Hakuna sheria inayokataza watu wasile mchana mwezi wa ramadhan ukiondoa sheria au imani ya dini ya kiislam.
“Ukweli wa tukio ni kwamba kulikuwa na vijana pale Mnazimmoja wanavuta bangi mchana na bahati nzuri aliyekuwa anarekodi video alizungumza watu wanavuta bangi mchana,” amesema CP Hamad na kuongeza:
“Kilichofanyika iliagizwa operesheni ifanyike wale wavuta bangi wakamatwe sababu ni kosa la jinai, hakuna sheria inaruhusu watu kuvuta bangi shida iliyotokea ni kwamba operesheni hiyo nadhani ilikamata waliomo na wasiokuwemo yaani wavuta bangi na waliokuwa wanakula mchana.”
Kauli hiyo ya Jeshi la Polisi Zanzibar, imekuja siku chache tangu Serikali ya Zanzibar ilaani kitendo cha watu kunyanyaswa kwa sababu ya kukiuka imani za dini ya watu wengine.
Hayo yanajiri baada ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Unguja, ACP Abubakar Khamis Ally, kusema wanawashikilia watu 12 kwa makosa ya kula na kunywa hadharani mchana wakati wa mwezi mtukufu wa Ramdhan.
Kamanda Ally alisema watu hao watafikishwa mahakamani kwa makosa ya kula na kunywa mchana hadharani.
Leave a comment