SPIKA wa Bunge, Dk. Tulia Ackson ameitaka Serikali kufanya tathimini ili kujua orodha ya wastaafu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyovunjwa 1977, ili walipwe mafao yao kama wanastahili. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Spika Tulia ametoa agizo hilo leo tarehe 2 Mei 2024, bungeni jijini Dodoma, katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Spika Tulia ameiagiza Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, washughulikie suala hilo ili ambayo hawajalipwa walipwe na kama wote wamelipwa wafahamishwe kama hakuna wanachodai.
“Sasa hili swali huwa linakuja linarejea, mi nafikiri upande wa Serikali ukaangalie kwenye nyaraka zake je wapo wanaodai? Kwa sababu nyaraka za waajiriwa wa kipindi hicho zipo watazame wote walishalipwa? Kama wako wanaodai walipwe kwa sababu haya maswali yanaendelea kurejea,” amesema Spika Tulia na kuongeza:
“Huenda wengine walifariki na haki zao zipo na wengine wapo huenda wanajipa moyo Kuna wanachodai kumbe hakuna, Bora mtazame ili mseme hakuna wanaodai.”
Spika Tulia ametoa agizo hilo baada ya Mbunge Viti Maalum, Hawa Mwaifunga, kuhoji kauli ya Serikali kuhusu malipo ya wastaafu hao kwani wamekuwa wakihangaika kwa muda mrefu kudai haki zao bila mafanikio.
Akijibu swali hilo, Waziri Majaliwa amesema wapo waliolipwa mafao yao na kwamba ambao bado wapeleke nyaraka zao kwa mwajiri wao ili walipwe stahiki zao.
Leave a comment