BAADA ya jitihada za kumtafuta Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana ya Chama cha NCCR-Mageuzi, Jovine Clinton, aliyepotea tangu tarehe 24 Januari 2023 kugonga mwamba, sasa Polisi wameamua kuanza kuchunguza simu zake ili kubaini mawasiliano yake ya mwisho.Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza kwa njia ya simu leo tarehe 30 Januari 2023, Mkuu wa Idara ya Uenezi na Mahusiano ya Umma wa NCCR-Mageuzi, Edward Simbeye, amedai kwamba Kituo cha Polisi Buguruni kimeamua kuhamisha uchunguzi wa suala hilo katika Idara ya Uchunguzi wa Kisayansi ya Jeshi la Polisi (Forensic).
Amedai kuwa, uchunguzi huo unafanyika kubaini mawasiliano ya mwisho aliyofanya Jovine , kwa ajili ya kujua mtu gani wa mwisho kuzungumza naye na kama kuna jumbe za vitisho vya kiusalama alikuwa anatumiwa.
“Jovine hatujampata mpaka sasa, tuko Kituo cha Polisi Buguruni tulikofungua jalada na kwa maelezo ambayo tumeyapata hapa wanahamisha taarifa yake kutoka kitabu cha taarifa kwenda kwenye jalada la uchunguzi la kisayansi ili wanaohusika na Forensic au uchunguzi wa simu waweze kufuatilia kujua tatizo liko wapi na kama kuna taarifa yeyote inayotupa mwanga kujua yuko wapi,” amesema Simbeye.
Aidha, Simbeye amedai kuwa kuna tetesi ya kwamba Jovine kabla ya kupotea alikuwa anapokea jumbe za vitisho kutoka kwa baadhi ya watu ambao hakuwataja.
“Tuko tunaendelea kufuatilia na ikifika saa 10 jioni tutashauriana kama tunapaswa kutoa taarifa tulizokuwa nazo kwa umma au kuwakabidhi Polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi,” amesema Simbeye.
Tukio hilo linajili wakati chama hicho kikiwa kwenye mgogoro wa kiungozi ulioibuka baada ya Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia pamoja na sekretarieti yake ya uongozi kung’olewa madarakani Mei 2022.
Mbatia na wenzake wakiwemo baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya NCCR-Mageuzi wanaodaiwa kuvuliwa wadhifa huo, wamefukua kesi kadhaa katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu ya Dar es Salaam, kupinga hatua hiyo kwa madai kwamba walifukuzwa kinyume cha sheria.
Kwa mujibu wa Simbeye, mara ya mwisho Jovine alionekana mahakamani hapo wakati akishiriki kesi ndogo Na. 570/2023 iliyofunguliwa na wajumbe wa zamani wa Bodi ya Wadhamini ya NCCR-mageuzi, kupinga uteuzi wa wajumbe wapya.
Leave a comment