JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, linamshikilia Selemani Malima, anayetuhumiwa kwa mauaji ya mke wake, Husna Mjaliwa, kwa sababu ya mgogoro wa kifamilia. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 19 Julai 2022, na Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, ACP Jumanne Muliro, ikiwa ni takribani mwezi mmoja tangu mtuhumiwa huyo kudaiwa kutoroka baada ya kufanya mauaji ya mke wake, tarehe 12 Juni mwaka huu.
Kamanda Muliro amesema kuwa, mtuhumiwa huyo alikamatwa tarehe 18 Julai 2022, maeneo ya Mbande jijini Dodoma, alikokuwa amejificha.
“Jeshi la Polisi limemkamata Malima aliyekuwa mkazi wa Keko Mwanga, kwa tuhuma za mauaji ya mke wake Husna aliyekuwa mkazi wa Goba, kwa kumchoma na kitu chenye ncha kali tumboni, lililotokea tarehe 12 Juni 2022 na mara baada ya tukio hilo alitoweka,” amesema Kamanda Muliro na kuongeza:
“Baada ya mahojiano ya kina, mtuhumiwa ameonesha kisu alichotumia kumuua mke wake. Uchunguzi wa shauri hili unakamilishwa na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani haraka iwezekanvyo.”
Leave a comment