WAKALA wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), umesema kufikia mwishoni mwa mwezi huu miradi maji 172 inayojengwa na fedha za Uviko-19 itakuwa imekamilika na wananchi 1,036,071 kupata huduma ya maji. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumanne tarehe 19, Julai, 2022 na Mkurugenzi Mkuu wa Ruwasa, Mhandisi Clement Kivegalo akizungumzia mafanikio ya mamlaka hiyo tangu kuanzishwa kwake na mipango ya mwaka huu wa fedha.
Amesema kupitia mpango wa UVIKO Serikali ilitoa fedha ambapo Ruwasa ilitengewa Sh 78.53 bilioni na kupitia fedha hizo imetekeleza miradi 172.
“Hadi Juni miradi 68 ilikuwa imekamilika na iliyobaki inatarajiwa kukamila mwezi huu na wananchi 1,036,071,” amesema.
Kivegalo amesema mambo ambayo yalikuwa changamoto katika sekta ya maji vijijini ni gharama kubwa ya ujenzi wa miradi ambayo hata hivyo ilikuwa haitoi huduma.
“Mara nyingi kilio kilikuwa uhalisia wa gharama za kwenye vitabu na mradi unavyoonekana kwa macho,” amesema na kuongeza;
“Tumeona hili ni jambo la kulikabili kwasababu linapunguza kasi ya Serikali kuendelea kuwapatia huduma ya maji wananchi.”
Kutokana na hali hiyo amesema katika mwaka wa fedha uliopita walitangaza zabuni ya miradi 86 na kulipata fursa ya kujadiliana na wakandarasi.
“Bei kabla ya majadilinao ilikuwa Sh367.3 bilioni lakini baada ya majadilinao gharama zilipungua hadi Sh309.9 bilioni na kuokoa Sh57.4 bilioni,” amesema Mhandisi Kivegalo
Leave a comment