KATI ya wanakwaya 24 ambao wameripotiwa kufariki dunia kutokana na ajali mbaya ya basi iliyotokea katika mto wa Enziu, eneo la Mwingi huko nchini Kenya, 22 walikuwa waumini katika kanisa la St. James Good Shepherd Catholic Church. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea).
Ujumbe wa mawasiliano uliotumwa kwa wanachama wa kanisa hilo ambao pia umenukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini humo umebainisha kuwa waumini hao walikuwa wanavuka mto huo kuelekea upande wa Nuu kuhudhuria harusi ya ndugu wa Padre Benson Kityambu wa kanisa la Katoliki la Mwingi.
Padre Kityambu anaripotiwa kupoteza wapwa wake 11 katika ajali hiyo jana tarehe 4 Disemba, 2021 muda wa saa saba mchana.
Ndugu wawili wa kidini ambao walikuwa wanafanya kazi katika seminari pia walipoteza maisha yao kwenye ajali hiyo.
“Wapendwa waumini na marafiki wa St.James, habari za jioni? Niruhusu niwataarifu kwamba kwaya yetu ya Kanisa Katoliki ya Good Shepherd-Mwingi leo (jana) walipata ajali mbaya ya barabarani wakielekea kuhudhuria harusi ya kaka yake Fr Benson Kityambu huko Nuu.
“Dereva alipokuwa akijaribu kuvuka mto Enziu, basi la St. Joseph Seminary lilipoteza mwelekeo na kusombwa kutokana na nguvu za maji. Mpaka sasa tumepoteza wanachama 22.
“Milli mingine bado inatafutwa. Wengine wameokolewa na kukimbizwa hospitali ya Mwingi level 4. Padre Kityambu amepoteza wapwa 11.
“Pia tumepoteza ndugu wawili wa kidini wanaofanya kazi katika seminari. Wapendwa tuendelee kuwaombea mahali pema peponi roho za marehemu,” ujumbe ulisoma.
Wakati shughuli za uokoaji zinasimamishwa jana jioni, tayari watu 24 walithibitishwa kufariki huku wengine 12 wakiokolewa.
Wanne kati ya 12 waliookolewa ni watoto huku wengine nane wakiwa watu wazima. 15 kati ya waliopoteza maisha ni kutoka familia moja.
Harusi ambayo ilikuwa ifanyike eneo la Nuu haikuendelea kufuatia msiba huo.
Timu ya waokoaji kutoka Jeshi la wanamaji nchini humo, Kenya Navy linasaidia katika kutafuta shughuli ya uokoaji.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Kaunti hiyo, Leah Kithei, amesema miongoni mwa walioathiriwa ni familia ya bi harusi, inayojumuisha watoto watatu na wajukuu wawili.
Mmoja wa waliookolewa ni Christopher Musili, 27, ambaye alieleza kuwa walikuwa zaidi ya abiria 65 kwenye basi hilo.
Hata hivyo, Musili alieleza kuwa baadhi ya watu waliokuwa ndani walikuwa wakijaribu kupasua madirisha ili waweze kutoka nje.
Rais Uhuru Kenyatta, Naibu Rais William Ruto, Raila Odinga, Kalonzo Musyoka na viongozi wengine wengi wameomboleza waliofariki na kutuma salamu za pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao.
Leave a comment