Klabu ya Soka Simba imefuzu kwenda hatua ya makundi katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika licha ya kuambulia kipigo cha bao 2-1, kutoka kwa wenyeji wao Red Arrows ya Zambia. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Simba imefanikiwa kuchanga karata zake vizuri katika mchezo huo wa marudiano ambapo mchezo wa awali ambao ulipigwa katika dimba la Mkapa jijini Dar es Salaam, Simba iliwachabanga Red Arrows bao 3 -0, hivyo Simba imesonga mbele kwa jumla ya mabao 4-2.
Katika mchezo wa leo tarehe 4 Disemba uliopigwa katika Uwanja wa Taifa wa Mashujaa jijini Lusaka nchini Zambia, wenyeji Red Arrows ndio walikuwa wa kwanza kuliona lango la Simba dakika ya 45 kupitia kwa Rick Banda aliyewazidi ujanja mabeki wa Simba na kufumua shuti lililomshinda mlinda mlango wa Simba Aishi Manula.
Baada ya kutoka mapumziko, Simba walishtushwa tena na bao la pili dakika ya 47 kupitia kwa Saddam Phiri hali iliyozidisha mashambulizi na presha kubwa langoni kwa Simba.
Kutokana na mashambulizi hayo kuzidi, Kocha wa Simba, Pablo Franco Martin alizidi kuimarisha safu yake ya ulinzi baada ya kumtoa kiungo mshambuliaji Benard Morrison na kumuingiza kiungo mkabaji Shomari Kapombe.
Hali hiyo ilisaidia kuiamsha Simba na kupata bao dakika ya 67 kupitia kwa Hassan Dilunga aliyefaidika na uzembe wa mabeki wa Red Arrows na kuingiza kamba mpira kwa kupitia angle ngumu ya kulia.
Bao hilo liliizidishia Simba nguvu ya kulinda faida ya wingi wa mabao kwani Kocha wa wekundu hao wa Msimbazi aliwaingiza beki kisiki Josh Onyango na Mzamiru Yassin, wakati katikati akitolewa Rally Bwalya.
Leave a comment