Monday , 6 May 2024
Home Habari Mchanganyiko NMB yaweka wazi inavyochangia maendeleo Zanzibar
Habari Mchanganyiko

NMB yaweka wazi inavyochangia maendeleo Zanzibar

Spread the love

 

BENKI ya NMB imeweka bayana ushiriki wake katika kutekeleza ajenda ya maendeleo Visiwani Zanzibar kwa kufadhili harakati za kuboresha maisha na shughuli za uzalishaji kwa njia kadhaa ikiwemo kuwekeza sehemu ya faida yake kwenye miradi ya kijamii. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea). 

Taasisi hiyo imesema mwishoni mwa wiki lililopita kwenye kilele cha wiki ya Tamasha la Kizimkazi kuwa mbali na huduma bunifu za kibenki pia inachangia ustawi wa visiwa vya marashi ya karafuu kupitia mipango kama ushirika wa kibiashara na kukuza utalii.

Akizungumza kwenye hafla ya Siku ya Kizimkazi Jumamosi, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuja na wazo la tamasha hilo ambalo alisema linazidi kukua na kuvutia watu wengi likitoa fursa za kiuchumi na maendeleo ya kijamii.

“Tunajivunia kuwa mshiriki mkubwa wa maendeleo ya hapa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla na tunaahidi kuendelea kujitoa zaidi kwa maslahi makubwa ya taifa letu,” alisema Zaipuna akiwambia Rais Samia aliyekuwa mgeni rasmi na kuipongeza NMB kwa mchango wake hasa ukopeshaji wananchi wa kawaida.

Mkuu huyo wa nchi aliyeambatana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliwachagiza Wazanzibari kuchangamkia huduma za NMB, ambayo ndiyo iliyokuwa mdhamini mkuu wa siku ya tamasha hilo, na hasa mikopo ambayo alisema zaidi ya kutohitaji dhamana lakini pia inapatikana hadi kwa kiasi cha Sh 5,000. 

“Tunajivunia zaidi uwezo wetu mkubwa na ubunifu wa kiteknolojia kutoa masuluhisho na kuwahudumia watanzania popote walipo yaani ndani na nje ya nchi,” alisema Zaipuna.

Aidha, alisema NMB imefanya makubwa katika sekta ya utalii ikiwemo kushirikiana na wadau kama ZATO na HAT ambavyo ni vyama vya waongoza watalii na wamiliki wa hoteli lengo likiwa ni kuhakikisha wageni wanapata huduma bora za kifedha.

NMB imefanikiwa katika hilo, alifafanua, na imekuwa benki ya kwanza nchini kuleta mashine za kubadilisha fedha za kigeni zinazowawezesha watalii na wananchi wengine kubadili hadi dola za Kimarekani 2,000. Zaipuna alisema ATM hizo tayari zipo kwenye viwanja vitatu vya kimataifa nchini ukiwemo ule wa Abeid Amani Karume.

Zaipuna alisema NMB imekuwa mdau mkubwa wa Tamasha la Kizimkazi ambalo aliahidi wataendelea kulidhamini na mshirika mkubwa wa shughuli za kijamii kwenye hasa nyajnja za ujasiriamali, elimu na afya.

“Mkuu wa Mkoa tayari amebainisha vizuri mchango wetu katika hilo lakini ngoja niongeze kidogo kwa kusema kuwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita tumetoa misaada yenye thamani ya zaidi ya TZS millioni 268 kwa shule 32 na vituo vya afya 28 hapa visiwani Zanzibar, yaani Unguja na Pemba,” kiongozi huyo aliimbia hadhira hiyo.

“Kama kauli mbiu ya mwaka huu inavyosema, Royal Tour na Uchumi wa Bluu ni Chachu ya Maendeleo, NMB tayari imetekeleza programu ya mafunzo kwa wakulima wadogo na tayari tumeshatoa elimu kwa wananchi karibia 3,800 ikiwemo vikundi zaidi ya 50 vya akinamama wanaojishughulisha kwenye sekta ya uvuvi, kilimo cha mwani na chumvi pamoja na kuwakopesha.”

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Rashid Khalid Rashid, alisema wakazi wa mkoa huo wana thamini ushiriki wa NMB kwenye maendeleo yao na benki hiyo imekuwa mdau nyeti wa maendeleo ya Zanzibar yote. 

Aidha, alisema uwekezaji wake kwenye shughuli za kijamii siku za hivi karibuni ni pamoja na vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya TZS milioni 17 katika skuli ya Kizimkazi Mkunguni, visaidizi vya walemavu vya TZS milioni 10 na kutoa TZS milioni 19.9 kujenga jengo la skuli ya Ndijani. 

“Pia NMB imetoa mafunzo kwa wanawake 500 na ina mpango wa kutoa mashine 50 za kukusanya mapato ya utalii na tayari vifaa hivyo 12 vinatumika kwa ajili ya majaribio. Tayari tumefanya mazungumzo nao kuona jinsi watakavyotoa mikopo ya kununua boti za uvuvi na kusafirisha watalii,” Bw Rashid aliongeza. 

Tamasha la Kizimkazi lilianza mwaka 2015 likijulikana kama Siku ya Samia na kubatizwa jina lake la sasa na kuwa na hadhi ya sasa hvi mwaka uliofuata ambapo limekuwa la kitaifa zaidi la kuchochea maendeleo na kukuza uchumi jumuishi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Mahakama yatoa uamuzi zuio dhidi ya Club House

Spread the loveMAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu jijini Dar es Salaam,...

Habari Mchanganyiko

GGML, OSHA yawanoa bodaboda 200 Arusha

Spread the loveZAIDI ya madereva bodaboda 200 wa jiji la Arusha wamepatiwa...

BiasharaHabari Mchanganyiko

Serikali kuwakopesha wajasiriamali 18.5bn/- kupitia NMB

Spread the loveSerikali imetenga kiasi cha Sh 18.5 bilioni kwa ajili ya...

AfyaHabari Mchanganyiko

Huduma za kibingwa zazinduliwa katika hospitali za halmashauri 184

Spread the loveSERIKALI imezindua huduma za matibabu za kibingwa katika hospitali 184...

error: Content is protected !!