NCHI ya Japan kupitia Ubalozi wake nchi Tanzania imetoa msaada wa Dola za Marekani 500,000 kwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa ajili ya kusaidia wakimbizi 204,000 kutoka Burundi na DR Congo katika kambi za mkoa wa Kigoma. Anaripoti Selemani Msuya, Dar es Salaam … (endelea).
Msaada huo wa Japan kwa WFP umetolewa jana na Balozi wa Japan, Yasushi Misawa, mbele ya Mkurugenzi na Mwakilishi wa WFP nchini Sarah Gordon-Gibson katika makazi ya balozi huyo jijini Dar es Salaam.
“Japan ni muungaji mkono mkubwa wa WFP duniani kote na inashukuru kwa jukumu la shirika hilo katika kukabiliana na mahitaji ya watu walio katika mazingira magumu hivyo ninafurahi kutoa mchango huu kwa niaba ya serikali na watu wa Japan kwa Tanzania,” alisema.
Balozi huyo alisema msaada huo utasaidia kukidhi mahitaji ya dharura ya chakula kwa watu walio katika mazingira magumu, hasa wakimbizi.
Misawa alisema mchango wa Japan katika kuunga mkono mwitikio wa kibinadamu wa WFP utasaidia kuhakikisha wakimbizi walio katika mazingira magumu nchini Tanzania wanaweza kukidhi mahitaji yao ya kilishe.
Alisema serikali ya Japan imekuwa ikitoa msaada wa chakula cha binadamu kwa nchi zinazoendelea tangu mwaka 1968 na ni mshirika wa muda mrefu wa WFP nchini Tanzania.
Mkurugenzi na Mwakilishi Mkazi wa WFP Gibson alisema mchango huo utatumika kununua tani 260 za maharage kwa ajili ya kikapu cha chakula cha shirika hilo, ambacho kina nafaka, mchanganyiko wa ngano iliyoongezewa nguvu na soya na sukari (Super Cereal), kunde, mafuta ya mboga na chumvi.
“Uhaba mkubwa wa fedha katika miaka ya hivi karibuni umeilazimu WFP kupunguza mgano kwa wakimbizi katika kambi za Nyarugusu na Nduta, wakati mwingine hadi theluthi mbili ya mahitaji yao ya chini ya kalori za kila siku, jambo ambalo lina athari mbaya kwa afya na ustawi,” alisema.
Alisema WFP inaishukuru Japan kwa mchango huu uliotolewa kwa wakati unaofaa ambao umekuja katika wakati muhimu ukizingatia mazingira magumu yaliyopo.
Gibson, alisema mchango huu utasaidia kwa kiasi kikubwa kuwekeza katika uchumi wa Tanzania kupitia ununuzi wa ndani wa maharage ambao hatimaye utazifikia kwa haraka kaya za wakimbizi walio katika mazingira magumu.
Alisema WFP ndilo shirika kubwa zaidi la kibinadamu duniani, linalookoa maisha katika hali ya dharura na kutumia msaada wa chakula kujenga njia kuelekea hali ya amani, utulivu na ustawi kwa watu wanaopata nafuu kutoka katika migogoro, majanga na athari za mabadiliko ya hali ya hewa.
Leave a comment