BENKI ya NMB imefikia makubaliano na Serikali ya Zanzibar kutunza bustani ya Forodhani Zanzibar ikiwa ni moja ya juhudi za kuunga mkono azma ya uhifadhi wa mazingira visiwani humo na ajenda ya uchumi wa bluu. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea).
Mradi huo wa utunzaji wa bustani ya Forodhani unalenga kuboresha mazingira ya kitalii na kuakisi vyema sifa maarufu ya eneo hilo.
Hatua hiyo itawezesha bustani hiyo kuvutia wageni wengi zaidi kila mwaka huku ukichangia kuchochea sekta ya utalii.
Akizungumza na waandishi wa habari visiwani Zanzibar wakati wa kutangaza Mashindano ya Mbio za Boti Zanzibar yanayodhaminiwa na Benki ya NMB, Mkuu wa Wilaya ya Mjini Magharibi, Rashid Simai Msaraka alisema NMB imekuwa mshirika mzuri wa maendeleo wa Serikali ya Zanzibar.
Alisema benki hiyo imekuwa mstari wa mbele kusaidia mipango mbalimbali ya maendeleo visiwani humo.
Mkuu huyo wa wilaya alisema Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan na Rais Hussein Mwinyi imekuwa ikiweka kipaumbele cha kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi na kuzitaka kampuni nyingi kuunga mkono mipango ya maendeleo ya Serikali.
“Tumefanya kazi kwa karibu sana na benki ya NMB katika miaka ya nyuma na nimedhihirisha na kutangaza kuwa tayari tumefikia makubaliano na Benki ya NMB ya kuendeleza na kutunza bustani za Forodhani hapa Zanzibar,” alisema Msaraka
Alisema pamoja na kuboresha mandhari ya eneo hilo, mradi huo utaleta manufaa makubwa nakusema, wakandarasi wazawa watazingatiwa huku akionyesha matumaini kuwa mradi huo utasaidia kuboresha sura ya Zanzibar.
“Tuna matumaini makubwa kuwa mbali na kutengeneza nafasi za kazi, mradi huu utasaidia kupendezesha na kuimarisha jiji letu kwa sababu eneo hilo ni mojawapo ya vivutio vikubwa hapa Zanzibar,” alisema.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Kadi wa NMB, Phillbert Casmir wakati wa hafla hiyo alisema dhamira ya benki hiyo katika kusaidia ushirikishwaji wa fedha na kuongeza kuwa benki hiyo itaendelea kutoa bidhaa zinazokidhi matakwa ya wateja.
Alisema mipango ya benki hiyo ni kuendelea kupeleka huduma karibu na wateja huku akiongeza benki hiyo ina mpango wa kupeleka huduma kwenye maeneo ya Wete, Nungwi, Mkoani, Uwanja wa ndege miongoni mwa maeneo mengine visiwani humo.
Katika hatua nyingine, benki ya NMB kwa kushirikiana na kampuni ya bima ya Britam Insurance wamedhamini mbio za boti za Zanzibar za mwaka huu.
Kampuni hizo mbili zitatoa zawadi kwa washindi zinazofikia Sh.6.5 milioni na zitatoa kifurushi cha bima ya ajali na kifo kwa washiriki wote kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Leave a comment