KAIMU Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Said Maditto, ameyataka Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) na Asasi za Kiraia, kufikisha malalamiko yao serikalini ili yatafutiwe ufumbuzi, badala ya kwenda kulalamika katika vyombo vya habari. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya … (endelea).
Maditto ametoa maagizo hayo hivi karibuni, ofisini kwake jijini Mbeya, alipotembelewa ujumbe wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), ulioongozwa na Meneja Program wake, Remmy Lemma.
“Niombe asasi ambazo ziko eneo hili, suala la kuimarisha mahusiano na majadiliano iwe kipaumbele kuliko kushutumiana. Wewe umeona kuna kitu kimetokea kule ulipo kuna Serikali, tafuta taarifa ya upande wa pili kujua limetokeaje kabla ya kushutumu au kwenda kwenye vyombo vya habari kulalamika. Haisaidii bali inaongeza chuki. Tuimarishe majadiliano,” amesema Maditto.
Wakati huo huo, Maditto amezitaka asasi za kiraia na NGO’s, kufuata sheria kwa kutekeleza masharti ya usajili wake, ili kuimarisha misingi ya utawala bora.
“Jambo la kwanza ninalowaagiza, mtekeleze matakwa ya sheria mliyosajiliwa nayo. Ni muhimu mkazingatia jambo hili maana ni la msingi na litaimarisha utawala bora, kwa sababu kama unatetea haki za binadamu halafu mwenyewe huzingatii inakuwa si vizuri,” amesema Maditto.
Pia, Maditto amezitaka asasi hizo ziwasilishe taarifa za robo mwaka, zinazoonesha utekelezaji wa majukumu yake.
Naye Remmy ambaye yuko mkoani Mbeya kwa ziara ya kikazi, kwa ajili ya kutembelea wanachama wa THRDC Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, amesema ziara hiyo ina lengo la kuangalia utendaji wa taasisi hizo.
Leave a comment