MAHAKAMA ya Uhalifu wa Kivita (ICC), imemkuta na makosa 61 kati ya 70 aliyotuhumiwa Dominic Ongwen, aliyekuwa mpiganaji wa kundi la waasi la LRA la nchini Uganda. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Mahakama hiyo leo Alhamisi, tarehe 6 Mei 2021, imeeleza kwamba itatoa adhabu ya kifungo kwa Ongwen siku zijazo, huku taarifa zaidi zikidai anaweza kukabiliwa na kifungo cha maisha gerezani.
Hata hivyo, mbele ya mahakama hiyo, Ongwen amejitetea akisema, LRA lilimlazimisha kula maharage yaliyolowekwa pamoja na damu ya mtu wa kwanza aliyemuua mwenyewe akiwa na miaka tisa, ilimvuruga.
Taarifa zaidi kutoka ICC zinaeleza, mawakili wa Ongwen wanajaribu kuhakikisha mteja wao anapata adhabu ndogo kwa kuwa, alikokotwa na kuingizwa kwenye jeshi hilo la waasi akiwa na umri mdogo – miaka tisa.
Miongoni mwa makosa aliyokutwa nayo ‘muasi’ huyo mwenye umri wa miaka 45, ni pamoja na ubakaji, kukamata watoto na kuwaingiza jeshini na mauaji.
Ongwen ambaye alitwaliwa na jeshi la Joseph Kony na kulazimishwa kutumikia jeshi hilo, na baadaye kuwa kamanda wa ngazi ya juu, anatuhumiwa kufanya mauaji kwa watu wasio na hatia.
Colin Black, mwendesha mashtaka ameeleza, Ongwen anaweza kukabiliwa na kifungo kisichopungua miaka 30, wakati walioathiriwa na uongozi wa ‘muasi’ huyo nchini Uganda wakitaka afungwe kifungo cha maisha.
Februari 2021, Jaji alisema Ongwen aliamrisha askari wake kufanya mauaji makubwa ya zaidi ya watu 130 katika kambi za wakimbizi za Lukodi, Pajule, Odek na Abok kati yam waka 2002 na 2005.
“Raia waliingia taharuki majumbani mwao kutokana na wengine walichomwa moto mpaka kufa, ama kufa kutokana na kipigo, wanawake walibakwa na kulazimshwa kutoa Watoto wao ili wajiunge na kundi hili,” alisema jaji huo.
Katika utetezi wake, Ongwen aliiambia ICC kwamba ni LRA ndio walimlazimisha kujiunga nao akiwa na umri mdogo wa kushindwa kutambua uzito wa kile alichokifanya baadaye.
Amesema, LRA lilimlazimisha kula maharage yaliyolowekwa pamoja na damu ya mtu wa kwanza aliyemuua mwenyewe akiwa na miaka tisa.
“Nipo mbele ya mahakama hii nikiwa na tuhuma nyingi, lakini bado mimi ni muathiriwa wa kwanza wa utotoni. Kilichotokea kwangu simaini hata kama kiliwahi kutokea kwa Yesu,” Ongwen amejitetea.
Mapema mwaka huu, ndugu zake Ongwen waliileza Al Jazeera kwamba, LRA lilikamata Watoto wengi wakati huo na kuwaingiza kwenye uasi.
“Tunasali asamehewe,” Johnson Odonga ambaye ni mjomba wake Ongwen aliiambia Aljazeera.
Kundi la waasi la LRA, lilianzishwa miaka 30 iliyopita na Kony ambaye alitangaza umwagaji damu Kaskazini mwa Uganda dhidi ya utawala wa Rais Yoweri Museveni.
Leave a comment