WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso amewasilisha bajeti ya wizara yake ya mwaka 2021/22 ya Sh.680.38 bilioni, ikiwa ni pungufu ya Sh.52.28 bilioni, ikilinganishwa na ya mwaka 2020/21 iliyokuwa Sh.733.28 bilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Aweso amewasilisha bajeti hiyo leo Alhamisi, tarehe 6 Mei 2021, jijini Dodoma.
Amesema, kati ya Sh.680.38 bilioni, matumizi ya kawaida ni Sh.33.75 bilioni, ambapo Sh.15.27 bilioni sawa na asilimia 45.2 ni kwa ajili ya kugharamia matumizi mengineyo (OC).
Aweso amesema, Sh.18.48 bilioni sawa na asilimia 54.8 ni kwa ajili ya kulipa mishahara (PE) ya watumishi wa wizara na Chuo cha Maji.
“Jumla ya bajeti ya maendeleo ni Sh.646.63 bilioni. Kati ya fedha hizo, Sh.346.63 bilioni sawa na asilimia 53.6 ni fedha za ndani na Sh.300 bilioni sawa na asilimia 46.4 ni fedha za nje,” amesema Aweso.
Awali, akizungumzia utekelezaji wa bajeti ya 2020/21, Aweso amesema, wizara hiyo iliidhinishiwa Sh.733.28 bilioni. Kati ya fedha hizo Sh.28.27 bilioni zilikuwa ni fedha za matumizi ya kawaida na Sh.705 bilioni zilikuwa ni fedha za maendeleo.
“Hadi mwezi Aprili 2021, wizara imepokea jumla ya Sh.396.77 bilioni sawa na asilimia 54.1 ya bajeti. Kati ya fedha zilizopokelewa, Sh.376.42 bilioni ni fedha za maendeleo sawa na asilimia 53.4 ya bajeti ya maendeleo,” amesema Aweso.
Waziri huyo amesema, kwa upande wa fedha za matumizi ya kawaida, jumla ya Sh.20.34 bilioni zilipokelewa sawa na asilimia 72 ya bajeti ya fedha za matumizi ya kawaida.
Leave a comment