RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametakiwa kuingilia kati mgogoro wa kiongozi uliobuka ndani ya Chama cha NCCR-Mageuzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Ijumaa, tarehe 23 Septemba 2022, jijini Dar es Salaam na Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Anthony Komu, akizungumzia hatua ya upande unaongozwa na Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Zanzibar, Haji Ambari, kuitisha kikao cha Halmashauri Kuu, licha ya kuzuiwa na mahakama.
“Tunajiuliza sana kwamba Rais sasa hivi ana mazungumzo yanayoendelea kati ya chama chake chini yake yeye na chama kikuu cha upinzani Chadema, kwa kile kinachoitwa kutafuta maridhiano. Sasa haya yanayoendelea ndani ya NCCR, ofisi yake haiyajui,” amesema Komu.
Komu amesema “ni kwa nini mkuu wa nchi ambaye ni mfariji mkuu anaona sisi tukiwa tunabaguliwa, tunaonewa, tunafedheheshwa kwa kiasi hiki anakaa kimya. Ni kwa nini watu wake wameshauriwa na watu wote hawa hakuna chochote kilichofanyika.”
Mnamo tarehe 7 Septemba 2022, Mahakama Kuu ya Tanzania, ilitoa zuio la muda la kufanya shughuli za chama kwa kambi inayodaiwa kufanya mapinduzi ya kiuongozi ndani ya NCCR-Mageuzi, hadi pale itakapotoa uamuzi dhidi ya kesi iliyofunguliwa na upande unaodaiwa kupinduliwa, unaongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, James Mbatia.
Mpo mahakamani. Huo sio muhimili wa utawala Raisi.