BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imetangaza kukamilika kwa taratibu ambazo zimewezesha Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kupata mkopo wa Dola za Marekani milioni 200 sawa na TSh. 470 bilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
NBC benki ni mwezeshaji mkuu ikishirikiana na benki ya NMB kama mkopeshaji mwenza katika kufanikisha upatikanaji wa mkopo huu mkubwa kwa Zanzibar.
Fedha zinazotokana na mkopo huo zitasaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii pamoja na miundombinu malengo yakiwa ni kuboresha maisha na hali ya kiuchumi kwa Wazanzibari.
Huu ni ushirikianao wa aina yake ambapo Benki ya NBC imeweza kufanya kazi na SMZ katika jitihada za kufanikisha miradi ya maendeleo kwa ustawi wa wananchi wa Zanzibar.
Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, amesema benki ya NBC inafurahi kusaidia upatikanaji wa mkopo huo utakaosaidia SMZ kufikia malengo yake ya ukuaji wa uchumi na maendeleo jumuishi.
Sabi amesema mkopo huo ni hatua kubwa na muhimu katika kushirikiana pamoja kwenye malengo ya maendeleo endelevu na kuboesha maisha ya wananchi wa kisiwa cha Zanzibar. Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa benki ya NBC itaendelea kuwa mstari wa mbele katika kusaidia jitihada za kuleta maendeleo ya kiuchumi kupitia huduma za kifedha.
Kwa upande wake, Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ally Mwinyi ameshukuru benki ya NBC kwa kufanikisha mkopo huo ambao amesema utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo Zanzibar na hivyo kukifanya kisiwa hicho kufikia malengo yake ya kuboresha maisha ya wananchi wake kwenye njanja za kijamii na kiuchumi.
Dk. Mwinyi ametaja baadhi ya maeneo ambayo yatanufaika na fedha hizo kuwa ni huduma za kiafya, elimu, miundombinu ya usafiri na miradi ya maendeleo ya kijamii.
“Kwa kuwekeza kwenye sekta hizi muhimu SMZ inalenga kuboresha maisha ya wananchi wake na kuongeza wigo wa upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii na kuwezesha kufikia malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya kiuchumi,” amefafanua
Leave a comment