KIONGOZI wa Kimila (Chifu) wa Zvimba, ametaka mwili wa aliyekuwa Rais wa Zimbabwe, Hayati Robert Mugabe (95), ufukuliwe kwa madai kwamba mazishi yake yalikuwa kinyume na mila za eneo hilo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Chifu Zvimba, amemtaka Mjane wa Mugabe, Grace Mugabe aufukue mwili huo kwa ajili ya kuzikwa upya, katika eneo lililochaguliwa na ndugu zake, akiwemo mama wa kiongozi huyo wa zamani wa Zimbabwe.
Mugabe aliyeiongoza Zimbabwe tangu 1987 hadi 2017, alipoondolewa madarakani kwa nguvu, alifariki dunia tarehe 6 Septemba 2019, kisha mwili wake ulizikwa tarehe 28 Septemba 2019, kijijini kwake Kutama, nchini humo.
“Katika barua yake kwenda kwa Grace, Chief Zvimba amemtaka mjane huyo aufukue mwili wa Mugabe ili uzikwe upya kulingana na tamaduni za watu wa Zvimba,” inaeleza taarifa ya mitandao hiyo.
Mbali na hilo, Chifu huyo kupitia barua yake kwenda kwa Grace, alimtaka mjane huyo wa Mugabe afike mbele ya mahakama ya kimila, kujibu tuhuma za kukiuka taratibu za mazishi hayo.
Pia, Grace ameamriwa kulipa ng’ombe na mbuzi kama fidia ya ukiukwaji huo.
Hata hivyo, leo Alhamisi tarehe 13 Mei 2021, Mpwa wa Mugabe, Patrick Zhuwao, amesema kiongozi huyo wa kimila hana mamlaka ya kuamuru mwili huo ufukuliwe, kwa kuwa mazishi yake yalifanyika kulingana na maagizo ya Mugabe aliyoyatoa akiwa hai.
Zhuwao amesema katika familia ya Mugabe hakuna mzozo wowote juu ya mazishi hayo.
Mugabe alizaliwa tarehe 21 Februari 1924, kwenye familia ya Washona, katika Kijiji cha Kutama wilayani Zvimba.
Leave a comment