MWANAJESHI wa Zambia amepandishwa cheo cha kijeshi kwa kumsaidia mwanamke mjamzito kujifungua mtoto katika shamba la mahindi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mwanajeshi huyo aliyefahamika kwa jina la Humphrey Mangisani amepadishwa cheo kutoka askari asiye na cheo hadi koplo kamili kwa ujasiri wake.
Kwa mujibu wa BBC, tukio hilo la mama huyo kujifungua lilitokea wiki iliyopita katika wilaya ya mashariki mwa nchi ya Petauke.
Koplo Mangisani alisema aliitwa kumsaidia mwanamke huyo ambaye alikuwa amepata uchungu wa uzazi.
Alimtafutia pikipiki ambayo ilimpeleka hospitali na kumfuata nyuma na bodaboda nyingine ili kufuatilia hali yake.
“Lakini uchungu wake ulikuwa wa haraka kiasi kwamba walilazimika kuweka kando pikipiki na kumsaidia kujifungua mtoto mchanga katika shamba moja la mahindi lililopo kando ya barabara.
“Nilitafuta na kupata wembe haraka na kumsaidia kukata kitovu. Mvua ilikuwa inanyesha alipojifungua. Nikamchukua mtoto haraka nikampeleka hospitalini na mama yake akafuata nyuma,” alisema.
Askari huyo nusura apatiwe adhabu kwa kuwa nje ya kambi lakini alipomueleza kiongozi wake tukio hilo, alisamehewa na kupongezwa.
Amesema mama huyo na mwanaye afya zao wote zinaendelea vizuri na alipewa fursa ya kutoa jina la mtoto na kumpatia jina la Raymond.
Pamoja na mambo mengine amesema awali walipewa mafunzo jeshini la kukabiliana na hali yoyote, hivyo tukio hilo lilipotokea kwake anamshukuru Mungu kwa kuwa wote wako salama.
Leave a comment