WIZARA ya Nishati imesema baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuagiza mgawo wa umeme usiwe mkali, wizara ilikaa na watalaam wake na kupata njia tatu za kupunguza makali ya mgawo huo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma leo tarehe 2 Februari 2022 wakati Naibu Waziri wa Nishati Stephen Byabato wakati akijibu swali la Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM).
Katika swali la nyongeza, Mpina amesema kukatwa kwa umeme kila mara na mgawo wa umeme unaoendelea hivi sasa, mwanzo ilielezwa ni sababu ya matengenezo ambayo hayakufanyika miaka mitano.
“Baada ya muda mfupi tukaambiwa ni kwa sababu ya mabwawa yanayotumika kufua umeme kukauka kwa sababu ya mifugo na ukaidi wa binadamu.
“Sasa hivi Tanesco wanasema hamna mgawo wa umeme, baadaye mgawo wa umeme unatangazwa…tuelezwe ukweli na serikali kwa sababu suala la katakata ya umeme, viwanda vinafungwa, wananchi wapo kwenye dhiki kubwa, huduma za afya, maji zimevurugika.
“Kiujumla taifa lipo kwenye hali ngumu ya ukosefu wa umeme tupate majibu sahihi ya serikali nini kinachosababisha hii katakata ya umeme,” amehoji Mpina.
Akijibu swali hilo, Byabato amesema sababu za kutokuwa na mgawo mkubwa ni baada ya wizara kukaa na watalaam kwa maelekezo ya Rais kwamba mgawo usiwe mkali kiasi kile.
“Tukabaini tunaweza kupata gesi iliyokuwa inapitia mitambo ya Payet ambao watakwenda kurekebisha mitambo yao, tukapitisha kiwango kidogo cha gesi kupitia mitambo ya TPDC na kufidia upungufu wa gesi ambao tungeupata.
“Ndio sababu ya kwanza kwamba lile pengo la gesi ambalo tungelipata tutapunguza kupitia kuchepusha gesi kupitia Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC),” amesema.
Sababu ya pili, Byabato amesema ni hali ya mabwawa ya kufua umeme kuanza kurudi katika hali nzuri na kuanza kujazia maji kwenye maeneo ambayo yanatakiwa yapate umeme.
“Tatu, umeme ni supply and demand, tulitarajia kutakuwa na mahitaji makubwa sana ya umeme. Tulifanya kitu kinaitwa load flow analysis, tulipoifanya tumebaini kwamba kile ambacho kitahitajika, sicho.
“Tuliona tutahitaji zaidi ya megawati 280 – 300, lakini sasa tumeona zitakazohitajika ni kama Megawati 100 ambazo zipo hapa na pale.
“Kwa hiyo ule mgawo ambao tulitarajia utakuwepo kwa makali yale, hautakuwepo. Tutahakikisha watu wanaendelea kupata umeme,” amesema.
Amesema katika kipindi hiki ambacho kutakuwa na mgawo mdogo au kutokuwepo kwa umeme katika maeneo mbalimbali, wanapunguza mzigo katika njia za umeme, kukatia miti na mapori ambayo yamekuwa yakiangukia maeneo ya umeme.
“Tutaendelea kuboresha vituo vyetu vya umeme, jana tulifanya Muhimbili, leo Kunduchi na kesho kutwa tutafanya Ubungo. Baada ya wiki moja au mbili tunarudi katika hali nzuri,” amesema.
Aidha, amesisitiza Tanesco haikatikati umeme wala hakuna mtu aliyeajiriwa kwa ajili ya kukata umeme.
Amesema mifumo ya umeme inapozidiwa kutokana na matumizi makubwa ya umeme huzima yenyewe.
Ameongeza mitambo hiyo inapozima, watu nao hupunguza matumizi hivyo Tanesco wanapokwenda kuangalia tatizo na kuiwasha, huwa inakubali kuwaka na matumizi yakiongezeka tena inazima.
“Lakini sasa tunaongeza nguvu za mitambo ili kuhimili mahitaji tuliyokuwa nayo,” amesema.
Leave a comment