Mwalimu Maganga Japhet amesimamishwa kazi na Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) kutokana na tuhuma za utoro kazini na kukaidi au kukataa kutekeleza maelekezo halali ya viongozi wake. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Taarifa za kusimamishwa kwa Maganga ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), zimetolewa jana Alhamisi kupitia barua ya taarifa kwa umma iliyosainiwa na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Manispaa ya Temeke, Fransisca Mselemo.
Barua hiyo imeeleza kuwa, Maganga amesimamishwa kazi na Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Elihuruma Mabelya chini ya Tume ya Utumishi wa Walimu ambayo ndiyo yenye mamlaka ya nidhamu ya walimu.
Taarifa hiyo imeeleza uamuzi wa kusimamishwa kazi Maganga, ulifikiwa tarehe 5 Desemba 2023 ambapo kabla ya kusimamishwa, Maganga alikuwa Mwalimu wa Shule ya Msingi Tandika iliyopo jijini Dar es Salaam.
Awali, Maganga aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera na Rais Samia Suluhu Hassan ingawa ilielezwa kwamba hakuitikia uteuzi huo na kuendelea kusalia kuwa Katibu Mkuu wa CWT.
Pia hayo yanajiri wakati Katibu Mkuu huyo wa CWT na Rais wake, Leah Ulaya wakituhumiwa kutumia zaidi ya Sh bilioni saba katika maandalizi ya maadhimisho ya sherehe za siku ya Mwalimu Duniani pamoja na kumbukizi ya miaka 30 ya CWT yaliyopangwa kufanyika kitaifa tarehe 13 Disemba mwaka huu mkoani Mwanza.
Baadhi ya wanachama wa CWT wamepinga matumizi hayo makubwa ya fedha huku wengine wakienda mbali zaidi na kuwatuhumu viongozi hao kuchochea migogoro ndani ya chama hicho kiasi cha kusababisha baadhi ya wanachama kujiengua na kujiunga na vyama vingine.
Leave a comment