MHALIFU wa makosa ya mauaji na ubakaji kutoka Afrika Kusini, Thabo Bester amekamatwa jijini Arusha nchini baada ya kusakwa kwa muda mrefu toka alipotoroka kimiujiza gerezani. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo tarehe 8 Aprili 2023 na Jeshi la Polisi Tanzania katika ukurasa wake wa Instagram imesema Bester amekamatwa akiwa na wenzake wawili wakiwa jijini Arusha.
“Ni kweli makachero wetu wamewakamata Thabo Bester, Dk Nandira Magudumana na Zakaria Alberto na wanashikiliwa na Jeshi la Polisi.
“Taratibu za mawasiliano ya kisheria ya ndani nay a kimataifa zinaendelea kukamilishwa,” imesema taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa mtandao wa APANews, Waziri wa Sheria wa Afrika Kusini, Ronald Lamola amesema, Bester alikamatwa jijini Arusha Tanzania Ijumaa usiku pamoja na mpenzi wake wa Afrika Kusini, Nandipha Magudumana na mtu mwingine kutoka Msumbiji.
Alisema kukamatwa kwa Bester kuliwezekana kupitia ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi la Afrika Kusini, Jeshi la Polisi la kimataifa (Interpol) na polisi wa Tanzania.
Inaelezwa walionekana wakitoka Dar es Salaam na kufuatwa hadi walipofika Arusha. Ilibainika kuwa walikuwa na hati za kusafiria kadhaa na hakuna hata moja kati ya hizo ambayo imegongwa muhuri nchini Afrika Kusini na Tanzania.
Bester, ambaye alikuwa akitumikia kifungo cha maisha jela kwa mauaji, alitoroka katika Kituo cha Mangaung huko Bloemfontein Mei 2022 baada ya awali kuaminika kuwa alijiua kwa kujichoma moto.
Hata hivyo, mhalifu huyo ambaye alihukumiwa kifungo cha maisha jela mwaka 2012, ilibainika kuwa mwili uliochomwa moto uliopatikana katika chumba alichokua Bester haukuwa wa muuaji na mbakaji huyo.
Bester, anayejulikana kama ‘mbakaji wa Facebook’, alipatikana na hatia mwaka 2012 kwa kuwabaka wanawake wawili na kumuua mmoja, baada ya kuwarubuni kwa kutumia mtandao wa Facebook.
Leave a comment