TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI), imewataka watumishi wake kukwepa vitendo vya ukiukwaji wa maadili, ikiwemo kuwa madalali wa hospitali binafsi kwa kuwahamasisha wagonjwa kwenda katika hospitali hizo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo tarehe 27 Oktoba 2023 na Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Prof, Abel Makubi, katika kikao cha pamoja kati ya viongozi wa taasisi hiyo na watumishi, kwa lengo la kutathimini hali ya utoaji huduma, katika taasisi hiyo.
Kiongozi huyo wa MOI, amedai baadhi ya watumishi wa taasisi hiyo wamekuwa wakiwashawishi wagonjwa wanaofika kupata huduma, kwenda kwenye hospitali binafsi.
“Baadhi yenu wachache, msiwashawishi wagonjwa kuhama hospitali kama wameshafika MOI, ninyi si madalali, menejimenti haipo tayari kuona wagonjwa wanaokuja hapa kwa jina la MOI wanahamishwa kwenda kwingine ” amesema Prof. Makubi.
Aidha, Prof, Makubi amewataka viongozi wa MOI kuhakikisha watumishi walio chini yao wanafuata maadili, umahili na weledi wa taaluma zao kwa kuzingatia kanuni za utoaji huduma bora kwa wateja, ili kuboresha hali ya utoaji huduma kwa wagonjwa.
Kwa upande wake Mtaalam wa Huduma bora kwa wateja, Padre John Kasembo amesema pamoja na mazingira magumu wanayopitia wakati wa utoaji wa huduma, watumishi wa MOI hawana budi kuwa tayari kujitoa sadaka kwa kutoa huduma bora kwa wagonjwa.
“Kuweni tayari kubadilika na kujitoa sadaka ili wengine wafaidike na huduma yako, nataka niwaambie kuwa huduma bora kwa wateja ndiyo uchawi wenyewe katika huduma au biashara, jiulize ukifa ni nani atalia, acheni nyayo huku mkiomba Mungu awasaidie katika utume wenu,” amesema Padre Kasembo.
Leave a comment