MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Rosemerry Senyamule anatarajia kuongoza zoezi la usafi kesho tarehe 28 Oktoba 2023 utakaofanyika katika Barabara ya 7, 8 na 9 kwa kuzibua mitaro iliyoziba ikiwa ni mwendelezo wa utekelezaji wa usafi wa mazingira hususani kila jumamosi ya mwisho wa mwezi. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Afisa Mazingira Mkoa wa Dodoma, Dikson Kimaro amesema kuwa zoezi hilo litaanza saa 12:00 asubuhi likiwahusisha viongozi mbalimbali wa Jiji la Dodoma.
Kati ya viongozi wa Jiji la Dodoma ambao watahusika ni pamoja na mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabiri Shekimweli, Meya wa Jiji la Dodoma Prof.Davis Mwamfupe, Mkurugenzi wa Jiji pamoja na wakuu wa idara mbalimbali kutoka ofisi ya mkuu wa Mkoa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Kimaro amesema kuwa hatua hiyo ni mwendelezo wa kuhakikisha jiji la Dodoma linakuwa katika hali ya usafi na kuweza kulipa Jiji hilo hadhi ya kuwa Jiji pamoja na umuhimu wa kuwa makao makuu ya nchi kutokana na kupokea wageni wa aina mbalimbali.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari Kimaro amesema kuwa licha ya kuwepo taratibu za kufanya usafi kila jumamosi na jumamosi ya mwisho wa mwezi lakini wananchi wanatakiwa kuhamasishwa nankujenga utamaduni wa kufanya usafi bila kushurutishwa.
Amesema kuwa kila mkazi wa Mkoa wa Dodoma anatakiwa kutambua na kuzingatia umuhimu wa kufanya usafi nankutumza mazingira kwa kuanzia nyumbani kwake hadi katika sehemu yake ya kufanyia kazi.
Katika hatua nyingine Afisa huyo amehimiza ujenzi wa vyoo bora na kufanya usafi unaokidhi viwango kwa kile alichosema ni sehemu ya kukabiliana na adhari za magonjwa ya milipuko yanaweza kujitokeza wakati wa kipindi kinachotabiliwa na Mamlaka ya hali ya hewa nchini na kusabanisha mvua za El-Nino.
Leave a comment