RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema licha ya vifo vitokanavyo na uzazi na vya watoto chini ya umri wa miaka mitano, kupungua, bado watumishi wa afya wanapaswa kukaza buti ili kutokomeza vifo vya aina hiyo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa maagizo hayo leo tarehe 28 Oktoba 2023, jijini Dar es Salaam, akizundua ripoti ya utafiti wa afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria kwa 2022.
Mkuu huyo wa nchi amesema ripoti hiyo imebanisha vifo vitokanavyo na uzazi vimepungua kutoka vifo 530 kwa vizazi hai 100,000 (2015/16) hadi kufikia 104 kwa vizazi hai 100,000 (2022). Wakati vifo vya watoto chini ya umri wa miaka mitano vikipungua kwa asilimia 1, huku vifo vya watoto wachanga vikiwa 24 kati ya vizazi 1,000.
“Tukilinganisha na shabaha ya malengo ya maendeleo endelevu (SDG’s), imetuagiza mpaka ikifika 2030 vifo vitokanavyo na kina mama wakati wa uzazi visizidi 70 kwa vizazi hai 100,000. Sasa tuko 104 safari yetu mpaka 2030 tunaweza tukafikia hii shabaha,”
“Ndugu zangu madaktari, wakunga tusibweteke twendeni tukakaze mwendo vifaa vipo tukafanye kazi kuokoa uhai wa wenzetu,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha huduma ya afya ili kutokomeza kabisa vifo hivyo.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ametaja mikoa inayoongoza kwa kuwa na mimba za utoto, ikiongozwa na Songwe (45%), Ruvuma (37%), Katavi (34%), Mara (31%) na Rukwa (30%), huku akiitaja mikoa ya Dar es Salaam, Njombe na Ruvuma, kuwa viwango hivyo vimeongezeka.
“Mmelegeza wapi sijui, kajiangalieni muwalinde watoto wenu,” amesema Rais Samia.
Leave a comment