MBUNGE wa M’baiki Mashariki nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, Alfred Yekatom amekamatwa ndani ya bunge baada ya kufyatua risasi hewani, wakati wabunge wakijiandaa kumchagua spika mpya. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Tukio hilo limetokea jana Jumatatu, ambapo Yekatom alifyatua risasi wakati akijaribu kukimbia, lakini hakufanikiwa na kuishia mikononi mwa polisi.
Yekatom ambaye aliwahi kuwa kiongozi wa kijeshi na kikundi cha wapiganaji cha Anti-Balaka Militia kilichokuwa kinatetea jumuiya za wakristo dhidi ya kikundi cha wapiganaji wenye itikadi ya kiislamu-Seleka , alizua taharuki na kusababisha baadhi ya wabunge kukimbilia nje.
Bunge la Jamhuri ya Afrika ya Kati lilikuwa linamchagua spika mpya siku tatu baada ya kuondolewa Spika Karim Meckassoua, anayewakilisha mji wenye waislamu wengi wa Bangui.
Baada ya uwepo wa mapambano makali baina ya vikundi vya waislamu na wakristo nchini humo, Meckassoua alichaguliwa mwaka 2016 kuwa spika, kitendo kilicholeta matumaini kuhusu upatanisho wa taifa hilo.
Hata hivyo, taarifa zinadai kuwa, kisa cha kuondolewa Meckassoua ni kutokuwa na ushirikiano mzuri na Rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, Faustin-Archange Touadera ambaye ni mkristo.
Baada ya kuondolewa kwenye wadhifa huo, Meckassoua siku ya Jumapili alitangaza kwenda mahakamani kupinga hatua hiyo, akidai kuwa ilisukumwa na tofauti za kidini kwa kuwa watu 38 kati ya 41 waliopiga kura ya kumuondoa, walikuwa ni wakristo.
Leave a comment