REGINA Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum (CCM), ameihoji mkakati wa serikali wa kuongeza bajeti ili kuboresha elimu katika Vyuo vya Ufundi (VETA) mkoani Manyara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
“Je, lini serikali itaongeza bajeti ya kuboresha elimu katika Vyuo vya Ufundi (VETA), mkoani Manyara ili kuboresha utoaji wa Elimu ya Ufundi?” amehoji leo Jumatatu tarehe 8 Februari 2021 bungeni, jijini Dodoma
Akijibu swali hilo, Omary Kipanga, naibu waziri wa wizara ya elimu, sayansi na teknolojia amesema, serikali imekuwa ikiongeza wigo wa bajeti kwa ajili ya kutekeleza mipango mbalimbali ya kuboresha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi nchini.
“Mkoa wa Manyara ni moja kati ya mikoa inayonufaika na ongezeko hilo la bajeti. Katika kipindi cha mwaka 2018 – 2020, serikali imetumia kiasi cha Sh.1.92 bilion.”
“Kati ya fedha hizo, Sh.600 milioni zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu na Sh.505.15 milioni kununua nyumba za watumishi katika Chuo cha VETA Manyara (RVTSC), kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC),” amesema Kipanga.
“Na kwamba, katika Chuo cha VETA Gorowa, kiasi cha Sh.337.08 milioni kimetumika kwa ajili ya ujenzi wa karakana, ofisi ya utawala na madarasa.”
Kipanga amesema “vilevile, katika Chuo cha VETA Simanjiro, serikali imetumia kiasi cha Sh.223.98 milioni kwa ajili ya kununulia vifaa vya kufundishia na kujifunzia na kujenga bweni la wasichana.”
“Sh.259.27 milioni zimetumika kugharamia mafunzo ya muda mfupi katika vyuo vya VETA Manyara na Gorowa. Serikali itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya kuboresha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi katika Mkoa wa Manyara na mikoa mingine kwa ujumla kulingana na upatikanaji wa fedha,” amesema
Leave a comment