Mbunge wa Dodoma Mjini, Anthony Mavunde (CCM) amewataka viongozi wa dini kuhimiza amani, mshikamano na upendo miongoni mwa watanzania kwa ustawi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Mavunde ambaye pia ni waziri wa madini, ameyasema hayo leo ijumaa katika Msikiti wa Gaddafi Jijini Dodoma wakati akizungumza na kutoa sadaka ya mwezi mtukufu kwa masheikh na Maimamu wa kata 41 za Jimbo la Dodoma Mjini.
“Nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kushiriki katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan.
“Ninawashukuru viongozi wote wa dini kwa namna ambavyo mmekuwa mstari wa mbele kuleta utulivu kwa kuhamasisha amani,upendo,umoja na mshikamano miongoni mwa wanajamii,” amesema.
Aidha, amesema wamekubaliana na uongozi kuanzisha mashindano ya kila mwaka ya kusoma Quran na kwa mwaka huu atatoa zawadi ya Sh 10 milioni kwa washindi wa kusoma Quran.
“Leo nimefika hapa kama ilivyo ada kwa ajili ya kukabidhi sadaka yangu kwenu katika fungu hili la 10 ya mwisho,ninawatakia mfungo mwema,” alisema Mavunde.
Akitoa shukrani kwa niaba,Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Alhaj Mustafa Rajabu Shaban amemshukuru Mavunde kwa ushirikiano mkubwa kwa jamii ya waislamu mkoani Dodoma na kuwataka viongozi wa Dini kuliombea Taifa na viongozi wake wakiongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan
Leave a comment