MAMIA ya watu wamewasili katika maeneo ya Buguruni Sheli jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya kushiriki maandamano ya amani yaliyoratibiwa na Chama Cha Chadema kupinga miswada ya Sheria za uchaguzi na kudai katiba mpya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kusanyiko hilo la watu limetokea leo tarehe 24 Januari 2024, ambapo Chadema kinazindua maandamano hayo yasiyo na kikomo hadi Serikali itakapofanyia kazi madai yao.
Tayari Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe ameshawasili eneo la tukio kwa ajili ya kuongoza msafara huo kuelekea ofisi za Umoja wa Mataifa (UN), zilizoko maeneo ya Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Katika msafara huo Mbowe anatarajia kutembea kwa mguu akiwaongoza waandamanaji hao
Magari na bodaboda kutoka maeneo mbalimbali yameambatana katika msafara huo, huku kukiwa na vikundi vya ngoma.
Akizungumza katika maandamano hayo, Mbowe amesema Chadema hakijakataa kukaa katika meza ya mazungumzo na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), isipokuwa kimeamua kupambana kwa kuingia barabarani hadi madai yao yatakapofanyiwa kazi.
“Tutaandamana hadi Serikali itakaposikiliza malalamiko yetu. Sisi hatujakataa meza ya mazungumzo tulichokiamua sisi tutazungumza wakati tunatembea na tunapambana barabarani sababu tumepata nguvu ya kuandamana mazungumzo yataendelea kuwepo Chadema hatujawahi kukataa mazungumzo,” amesema Mbowe.
Maandamano hayo yameanza majira ya saa nne na nusu asubuhi ambapo Mbowe ameambatana nao ni John Mrema, Godbless Lema, Benson Kigaila, Sugu na wengine. Wanachama waliokuja kuandamana wametoka majimbo ya Temeke, Segerea, Mbagala na Ilala.
Leave a comment