Chama cha Chadema kimeibua shangwe kwa baadhi ya wananchi waliokuwa maeneo ya Buguruni jijini Dar es Salaam, huku Mwenyekiti wake Freeman Mbowe akiteka hisia za watu wengi. Anaripoti Regina Mkonde …(endelea).
Kila alipopita Mbowe na msafara wake leo tarehe 24 Januari 2024, wananchi wamekuwa wakimshangilia na kuonesha alama ya vidole viwili ya chama hicho huku wakimuita mwamba.
Baadhi ya wananchi waliokuwa pembeni wamesikika wakisema “waambieni lazima waseme, maisha magumu sana.”
Baadhi ya watu waliokuwa pembezoni mwa barabara ya Buguruni kuelekea Ilala Boma ikiwemo wafanyabiashara walilazimika kuacha biashara zao na kusogea karibu ya barabara kwa ajili ya kuwaona wanaoandamana.
Baadhi ya madereva wa bajaji na bodaboda waliokuwa wanaitumia barabara hiyo kuelekea maeneo mengine wamekuwa wakionesha ishara ya Chadema.
Mfanyabiashara mmoja wa soko la Buguruni ambaye anauza dagaa, jina hakupenda kutajwa alisema “sasa Tanzania ya amani imerudi, watu wanaruhusiwa kuandamana, huenda Serikali ikafanyia kazi malalamiko yao kwa kuwa Rais Samia anaonekana ni msikivu sana.”
Pamoja na mambo mengine sasa katika barabara ya Ilala kuna foleni ya magari inayosababishwa na maandamano hayo ambapo magari yanalazimika kusimama kwa muda ili kuupisha msafara wake.
Polisi wamekuwa wakiambatana na waandamanaji kwa ajili ya kuwalinda. Hadi sasa hakuna vurugu zozote zilizojitokeza au mtu kupata madhara.
Chadema wameitisha maandamano hayo ili kuishinikiza Serikali iondoe bungeni miswada ya sheria za uchaguzi kwa ajili ya kufanyiwa maboresho ili kuondoa dosari zilizoko katika mfumo wa uchaguzi.
Pia, kinaitaka Serikali ikamilishe mchakato wa upatikanaji katiba mpya pamoja na kuondoa ugumu wa maisha kwa wananchi uliosababishwa na mfumuko wa bei na kupanda kwa gharama za maisha.
Leave a comment