MKUU Mkoa wa Arusha, Paul Makonda amewataka watu wanaowatuma mawakala wao kumtukana mitandaoni Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, waache mara moja kwani wasipofanya hivyo atawaanika hadharani kwa kuwa ana majina yao wakiwemo mawaziri. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza katika kumbukumbu ya miaka 40 ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, hayati Edward Sokoine, leo Ijumaa jijini Arusha, Makonda amedai kuna watu wenye lengo la kumkatisha tamaa Rais Samia, hivyo anamuomba Mungu ampe ulinzi wa moyo wake ili aendelee kuwatumikia watanzania.
“Nakuombea kwa Mungu akupe wigo wa bullet proof itakayolinda moyo wako ututumikie sisi watanzania, nafahamu wenye maneno na hawaishi kusema maneno lengo lao ni kukukatisha tamaa tena wengine umetupa nafasi tumo ndani ya uongozi wako na nitumie fursa hii kuwaambia hasa kaka zangu mnaotuma na kulipa watu kumchokoza mama yangu Samia, mnanijua na ninyi nawajua,” amesema Makonda.
Makonda amesema “kwa majina yao nawajua na leo tarehe 12 nataka iwe mwisho kuwatuma watu hao wanaotukana kwenye mitandao ya kijamii. Ikiendelea Jumatatu nakutajia majina wengine mawaziri na wengine wanapewa nguvu na watu tunaowaheshimu, naomba iwe msiho tumuache afanye kazi aliyopewa na Mungu.”
Katika hatua nyingine, Makonda amemshukuru Kardinali Polycarp Pengo kwa kuwa naye karibu katika nyakati zote alipokuwa na cheo na hata alipokuwa hana cheo.
“Nitambue nafasi ya baba wangu na mlezi wangu wa kiroho Kardinali Pengo, mzee huyu ni wa tofauti sana nimekuwa naye kwa nyakati zote nilizopitia, nilipokuwa na cheo alikuwepo nilipokuwa sina cheo alikuwepo. Kwa hiyo ninapomuona amefika mahala hapa naiona heshima na upendeleo wa kimungu kukanyaga kwenye ardhi uliyonipa kuiongoza, ardhi haitazaa tena mapooza,” amesema Makonda.
Leave a comment