MHASHAMU Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha, Isaac Amani, ameiomba Serikali kupitia vyombo vyake vya dola kuwashughulikia watu wanaofanya ubadhirifu wa fedha za umma (mafisadi) kwa kuwa wanarudisha nyuma maendeleo ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es salaam…(endelea).
Askofu Amani ametoa wito huo leo tarehe 12 Aprili 2024, akiongoza misa maalum ya kumbukumbu ya miaka 40 ya kifo cha aliyekuwa waziri mkuu wa Tanzania, Hayati Edward Sokoine, jijini Arusha.
Kiongozi huyo wa dini amesema Hayati Sokoine enzi za uhai wake alipiga vita ufisadi na watu wanaohujumu uchumi wa nchi “Sokoine alikuwa mpiga vita wa uhujumu uchumi na waliomfahamu walimtambua kwa hilo mambo ya ufisadi.”
Askofu Amani amesema enzi za uhai wake Sokoine alipiga vita matumizi ya dawa za kulevya ikiwemo bangi (jani la Arusha) kwani matumizi ya dawa hizo yanarudisha nyuma maendeleo ya nchi na kuharibu afya ya akili ya wanaotumia hasa vijana.
“Leo angekua hai angetuambia tujihadhari sana na jani la Arusha, angesema haiwezekani tukawa na ustaarabu na maendeleo tusipojitenga na dawa za kulevya, vijana wanaangamia katika jambo hilo, wanaouza madawa hayo inafaa watafutwe washughulikiwe vizuri kisheria ili tuweze kuwa na maendeleo ya kweli na watu wenye akili timamu sio mazezeta,” amesema Askofu Amani.
Amesema Sokoine alikuwa mzalendo na shujaa wa nchi, aliyependa maendeleo ya taifa lake.
Katika hatua nyingine, Askofu Amani amewahimiza watanzania kuwa wazalendo katika kutoa kodi ili Serikali ipate fedha za kuwahudumia.
“Bwana Yesu alipotoa mikate watu walitaka kumfanya mfalme wa mikate, watu walipoona hiyo mikate tena ya bure walitaka awe mfalme wa mikate anatoa wanapokea, kumbe hapa kwetu Tanzania kwa njia ya kodi tunawezesha Serikali kufanya kazi. Tuna wajibu wa kulipa kodi na serikali ina wajibu pia kuhudumia wananchi,” amesema Askofu Amani.
Leave a comment