WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa, amesema uwepo wa upepo unaobadilisha mwelekeo mara kwa mara ni miongoni mwa changamoto za kukabiliana na moto Mlima Kilimanjaro. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Majaliwa ametaja changamoto hizo leo Alhamis tarehe 3 Novemba, 2022, bungeni jijini Dodoma wakati wa kipindi cha masawali na majibu kwa Waziri Mkuu.
Amesema sababu nyingine ni uwepo wa miinuko mikali na makorongo makubwa, uwepo wa mimea aina ya erica ambayo inashika moto kwa urahisi na mlindikano mkubwa wa mboji ambayo huifadhi moto kwa muda mrefu.
Hata hivyo amesema zoezi la kudhibiti moto katika maeneo hayo korofi linaendelea vizuri na mengi yameshadhibitiwa.
“Zoezi la uzimaji moto linaendelea vyema, moto umedhibitiwa kwa kiasi kikubwa katika maeneo korofi,”amesema.
Maajaliwa amewashukuru wadau mbalimbali ambao wanashirikiana na Serikali kuhakikisha moto huo unadhibitiwa na kuzimwa kabisa.
“Ninatoa shukrani za pekee kwa Jeshi la Wananchi Tanzania kutoa helkopta mbili na askari 878 kuongeza nguvu katika uzimaji wa moto ambao umedhibitiwa katika maeneo,”amesema.
Ametaja athari kadhaa zilizosabishwa na moto ni pamoja na uteketeza eneo la ukubwa wa kilomita za mraba 33 la uoto wa asili, kuteketeza viumbe mbalimbali na kuharibu mandhari ya ukanda wa juu wa hifadhi.
Amesema kutokana na jitihada za wadau waliweza kuokoa maeneo muhimu ya utalii ambayo yamebaki salama na hivyo shughuli za utalii kuendelea kama kawaida.
Majaliwa ameielekeza Wizara ya Mali Asili na Utalii kushirikiana na TANAPA na KINAPA kuhakikisha kuwa kinaundwa kitengo cha kukabiliana na majanga ndani ya hifadhi ili kuzuia changamoto za majanga mbalimbali.
Kuzuka kwa moto Mlima Kilimanjaro kuliripotiwa Oktoba 21, 2022 saa 2 usiku ambapo ulianzia eneo la bonde la Karanga na kusambaa maeneo mengine ya hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA).
Leave a comment