HATIMAYE majaji sita ambao walikuwa wameteuliwa na Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) nchini Kenya mwaka 2019 na majina yao kukataliwa na Rais mstaafu wa taifa hilo, Uhuru Kenyatta, wameapishwa. Anaripoti Helena Mkonyi, TUDARDCo … (endelea).
Majaji hao ni Weldon Korir, George Odunga, Aggrey Muchelule na Joel Ngugi wa mahakama ya rufaa na Evans Makori na Judith Omange wa Mahakama ya Mazingira na ardhi.
Kuapishwa kwa majaji hao kumejiri siku moja baada ya uteuzi wao kuidhinishwa na Rais William Ruto aliyeapishwa jana katika uwanja wa Kasarani jijini Nairobi nchini humo kushika wadhifa huo.
Ruto alichapisha majina ya majaji hao kwenye gazeti rasmi la serikali muda mfupi tu baada ya kuapishwa kuwa rais wa Kenya.
Akiwahutubia majaji hao Rais Ruto aliahidi kuheshimu uhuru wa idara ya mahakama.
Amesema atafanikisha mazungumzo ya kila iwapo kama kuna jambo lolote linalohusu idara hiyo ya mahakama.
Rais Ruto amesema lazima serikali ikabiliane na ukiukaji wa sheria na kutoa wito kwa wakenya kufahamu kuwa kila mtu anaongozwa na sheria na katika sheria hakuna upendeleo.
“Hata mimi kama rais nina kimo changu katika sheria na siwezi fanya jambo nje ya sheria, kila mmoja wetu anatakiwa kufuata sheria,” Ruto amesema.
Majaji hao walikuwa miongoni mwa wengine 40 walioteuliwa mwaka 2019 baada ya zoezi la kuhakikiwa na Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) kati ya Julai na Agosti mwaka huo.
Juni 2021, Rais mstaafu Uhuru aliteua majaji 34 lakini aliwaacha nje majaji sita akidai kuwa amewaacha kwa sababu ya masuala ya uadilifu.
Oktoba 2021 ikiwa ni siku chache baada ya Mahakama Kuu kuamuru Uhuru kuteua majaji waliosalia ndani ya siku 14, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Kenya, Paul Kariuki alikata rufaa dhidi ya uamuzi huo.
Leave a comment