KATIBU wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda, amewasilisha mapendekezo juu ya namna ya kuboresha mfumo wa haki jinai, huku akitaka taasisi zinazousimamia zipunguziwe mamlaka ili kulinda maslahi ya wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Sheikh Ponda amewasilisha mapendekezo hayo hivi karibuni, katika kikosi kazi kilichoundwa na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kuangalia namna bora ya kuboresha mfumo wa haki jinai nchini.
Katika mapendekezo hayo, Sheikh Ponda amedai Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), inakabiliwa na dosari mbalimbali, ikiwemo kuendesha zoezi la Plea Bargaining kinyume cha sheria na kuwafungulia mashtaka watu bila ushahidi kukamilika, kitendo kinachopelekea baadhi ya watuhumiwa kusota rumande bila kesi zao kusikilizwa, kwa maelezo ushahidi haujakamilika.
Kutokana na udhaifu huo, Sheikh Ponda ameshauri ofisi ya DDP ifanyiwe uchunguzi utakasaidia kutafuta muarobaini wa changamoto zake ili kiwe chombo huru.
Kiongozi huyo wa kiislamu, ameshauri masharti ya dhamana kwa watuhumiwa yawe mepesi, huku akishauri Jamhuri isiwe na fursa ya kubadilisha shtaka walilofungua mahakamani dhidi ya mtuhumiwa. Pia, ameshauri askari atakayetuhumiwa kuwa mtuhumiwa afikishwe mahakamani.
Kuhusu Jeshi la Polisi, Sheikh Ponda amedai taasisi hiyo inakabiliwa na changamoto ya baadhi ya watendaji wake kutumia nguvu, rushwa na ukiukaji wa haki za binadamu, ambapo ameshauri Serikali iajiri wataalamu wa ndani na nje watakaotoa mafunzo bora kwa askari polisi.
Aidha, Sheikh Ponda ameshauri wito wa watuhumiwa kufika polisi ufanyike kiraia kwa wahusika kuitwa kwa barua na kupewa uhakika wa kurejea nyumbani salama, maelezo ya kukataa au kukiri kosa kwa mtuhumiwa lisifanywe na Polisi bali lifanywe na mahakama, pamoja na mtuhumiwa kutokana mahabusu kwa zaidi ya saa 24.
Sheikh Ponda amegusia maboresho katika Jeshi la Magereza, akishauri huduma za mahabudu ziwe tofauti na wafungwa, pamoja na wafungwa na mahabusu kupatiwa milo kamili.
Ameshauri Serikali iandae muswada wa kuboresha Tume ya Haki za Binadamu, pamoja na kuifuta maboresho Sheria ya Ugaidi ya Tanzania ya 2002, akidai ina mapungufu.
Leave a comment