BARAZA la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), limesema kwa mara ya kwanza limeamua kutoka mstari wa mbele kutoa mapendekezo yake juu ya uboreshaji sheria za uchaguzi, kutokana na vyombo vinavyosimamia pamoja na mahakama kukosa uaminifu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Sababu hizo zilitajwa jana tarehe 8 Januari 2023, jijini Dodoma na mwakilishi wa TEC, Askofu Yuda Thadei Ruwai’chi, akiwasilisha mapendekezo ya baraza hilo kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria.
Askofu Rwai’chi amesema kabla ya uchaguzi wa vyama vingi vya siasa kufanyika 1995, tume iliyokuwa inasimamia suala hilo pamoja na mahakama, zilikuwa zinaridhisha watu kutokana na utendaji wake, lakini kwa sasa vyombo hivyo vimeonekana kukabiliwa na changamoto nyingi kiasi cha kushusha imani yake kwa jamii.
“Ikumbukwe kwamba, jinsi miaka ilivyokuwa ikienda mbele lilipokuja suala la kuchagua viongozi wetu uzoefu unatuonyesha kuwa tume imeonyesha kuwa na changamoto nyingi kiasi kwamba kuaminika kwake kumekuwa kunashuka kila kipindi cha uchaguzi. Sote tumeshuhudia malalamiko kutoka kwa wapiga kura, wagombea na makundi mbalimbali ya ndani na nje ya nchi,” alisema Askofu Ruwai’chi.
Alisema “kilichotushtusha ni jinsi ambavyo chaguzi za 2019 na 2020 zilivyosimamiwa na tume zilirudisha nyuma mafanikio ya kuratibu chaguzi maaskofu walisikitishwa sana kuona yaliyojiri na baada ya kutafakari hayo wakaona ni vyema kwa mara ya kwanza waje mbele ya kamati wajieleze watoe maoni yao na tahadhari yasije yakajitokeza yale tunayoyaona katika nchi nyingine za kiafrika kwenye masuala ya uchaguzi.”
Akitoa mapendekezo ya TEC kuhusu marekebisho ya Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), alisema wanapendekeza mamlaka ya Rais kuteua wajumbe wa tume yaondolewe badala yake wateuliwe na chombo huru na kuapishwa na jaji mkuu wa nchi au jaji wa mahakama ya rufaa.
Pia, Askofu Ruwai’chi alisema wanapendekeza NEC itengewe fedha katika bajeti ya utekelezaji wa majukumu yake, ili kuipa uhuru wa kifedha. Wanashauri Waziri wa Utumishi wa Umma asiwe na haki ya kuunda sekretarieti ya tume hiyo.
Mapendekezo mengine ni watumishi wanaothibitika kukosa uaminifu wa tume wafukuzwe kazi, mkurugenzi wa uchaguzi asisaidie majukumu yake na watumishi wa umma ili kukwepa chaguzi kuingiliwa pamojana NEC kuwa na watumishi wake wa kudumu ili iwe huru.
Leave a comment