TUNDU Lissu, mbombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameahidi kufuta sheria zote kandamizi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Ametoa ahadi hiyo jana Jumatatu tarehe 31 Agosti 2020, akiwa kwenye kampeni za kusaka urais zilizofanyika katika viwanja vya Relini, jijini Arusha.
“Tanzania ya Tundu Lissu baada ya tarehe 28 Oktoba, tutafanya marekebisheo makubwa katika mfumo wa kisheria kuhusu kesi za jinai na nitafanya haraka kabisa,” alisema Lissu.
Lissu ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Bara alisema, endapo atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania, atarekebisha mfumo wa sheria kuhusu kesi za jinai, ili kuondoa sheria zinazonyima watuhumuwa dhamana, hasa wa utakatisha fedha na uhujumu uchumi.
“Kitu kikubwa ambacho kinasababisha mateso haya ya makesi ya uongo chanzo kikubwa ni kwamba, kuna masheria ya ukandamizaji ambayo yametengeza makosa yasiyokuwa na dhamana, ukipigwa utakatishaji fedha unaozea gerezani hakuna dhamana,” alisema Lissu.
“Tanzania ya Tundu Lissu itafuta sheria zote zinazonyima watu dhamana, Katiba yetu inasema, mahali kila mtu anahesabika kuwa hana hatia hadi hapo hatia yake itathibitishwa mahakamani, maana yake kama Katiba inasema huna hatia, hutakaa gerezani sababu umetuhumiwa tu.”
Lissu aliahidi kuifuta machozi nchi ya Tanzania pamoja na kurudisha umoja wa wananchi hasa wa jiji la Arusha.
“Arusha ya ujana wangu ilikuwa Arusha ya amani, ilikuwa Arusha ya upendo na watu kusaidiana, Arusha ya leo ya watu ambao wanateswa kwa miaka mitano, wamenyang’anywa pesa zao.”
“Arusha ya leo ni ya machozi damu na vilio kwa sababu ya ukandamizaji wa miaka mitano, baada ya tarehe 28 Oktoba nitafuta machozi ya Arusha, nitafuta machozi ya Tanzania,” aliahidi Lissu.
Leave a comment