MGOMBEA urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli amesema, iwapo atapewa ridhaa na wananchi kuongoza Tanzani kwa awamu ya pili, kasi yake ya maendeleo itakuwa kubwa zaidi ya iliyopita. Anaripoti Mwandishi Wetu, Bahi … (endelea).
Ametoa kauli hiyo leo Jumanne tarehe 1 Septemba 2020, wakati akiomba kura wananchi wa Bahi, jijini Dodoma. Pia, amewaomba wananchi hao kuchagua wagombea wote wa CCM.
“Lakini mnichagulie madiwani hawa, naomba niwaahidi tutachapa kazi kubwa isiyo na mfano, hii miaka mitano ilikuwa ni onja onja, hii yenyewe ndio inakuja,” amesema Dk. Magufuli.
Amewataka wananchi wa Bahi na Watanzania kwa ujumla kushikama katika kipindi hiki cha uchaguzi ili kuhakikisha Taifa linabaki na amani.
“Ninawaomba tushikamane, lakini pia tulinde amani yetu ni kitu kikubwa katika maisha ya binadamu, pia tuchape kazi,” amesema Rais Magufuli.
CCM kinaendelea na kampeni zake za urais baada ya kuzindua Jumamosi tarehe 29 Agosti 2020, ambapo leo Dk. Magufuli anaendelea na kampeni mkoani Singida.
Mgombea huyo pia ameahidi kuleta maendeleo zaidi katika Mkoa wa Dodoma, endapo atafanikiwa kushinda uchaguzi huo.
“Huu ni wakati wa kampeni, tumeona turudi kwa umma nataka kuwaeleza wana Bahi, sasa hivi makao makuu ya nchi yetu yako Dodoma mimi mwenyewe nakaa Dodoma sitashindwa kufanya maendeleo sababu Bahi na Dodoma ni pua na mdomo nataka niwahakikishie ndugu zangu sitawaangusha,” ameahidi Rais Magufuli.
Leave a comment