MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Mzee Stephen Wasira, amesema Rais Samia Suluhu Hassan, ana kazi ya kufanya katika kukabiliana na mfumuko wa bei ya mafuta katika soko la dunia, uliosababishwa na vita kati ya Urusi na Ukraine. Anaripoti Mwadishi Wetu, Pwani … (endelea).
Mzee Wasira ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, tarehe 9 Aprili 2022, akizungumza katika mdahalo wa kitaifa wa kuadhimisha miaka 100 ya kuzaliwa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyere, iliyofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.
Waziri huyo wa zamani wa Tanzania, amesema licha ya Rais Samia kuwa na sera ya maendeleo ya watu, bado ana kazi ya kufanya katika kukabiliana na athari ya vita hiyo iliyoibuka mwishoni mwa Februari 2022.
“Wakati Rais Samia anajitahidi sana kwenda na sera ya maendeleo ya watu, kwa sababu maendeleo lazima yawe ya watu, ndiyo maana mkazo wake uko katika mifumo inayozingatia maendeleo ya watu. Lakini bado ana kazi ya kufanya, kuna Ukraine na Urusi inapandisha bei ya mafuta,” amesema Mzee Wasira.
Mzee Wasira amesema “ukienda mtaani wanadhani Samia ndiye anaanzisha vita, kwa hiyo wanasema kwa nini bei hasimamii, Samia atasimamia bei lakini hawezi kuzuia kupanda kwa mafuta, sababu Urusi inayopigana ni ya tatu kutoa mafuta duniani ikishindwa kuuza sababu ya vikwazo kuna kuwa na upungufu wa mafuta na bei zinapanda.”
Mwanasiasa huyo amesema, wanaohoji kwa nini Rais Samia hasimamii mafuta , anamtwisha mzigo.
“Kukiwa na upungufu wa mafuta duniani bei zinapanda, ukisema Rais Samia kwa nini hasimamii mafuta, hii sasa unamwtisha mzigo,lakini naamini kila tunapoendelea kujifunza, tunajua nani ni nani na nini ni nini,” amesema Mzee Wasira.
Leave a comment