KESI iliyofunguliwa na wabunge viti maalum 19 wakiongozwa na Halima Mdee, imeahirishwa hadi tarehe 18 na 19 Mei,2023 kutokana na Jaji anayeisikiliza, Cyprian Mkeha kuwa nje ya Dar es Salaam kwa majukumu mengine ya kikazi. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kesi hiyo leo Jumanne ilipangwa kuendelea kusikilizwa kwa Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Chadema, Ruth Mollel kuhojiwa na mawakili wa wabunge hao kuhusu hati kiapo walichowasilisha mahakamani hapo kujibu malalamiko yao ya kufukuzwa na chama hicho bila kusikilizwa.
Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya mawakili wa pande zote mbili kuitwa ‘chember Court’ na kuahirishwa kwa kesi hiyo, Wakili Peter Kibatala amedai kuwa kesi hiyo imeahirishwa mbele ya Msajili Wa Mahakama hiyo, Veronica Mteta.
“Msajili Wa Mahakama hii, Veronica Mteta ametuita (mawakili wa pande zote mbili) chumba namba 76, kama mlivyoona na kutueleza kuwa jaji ana majukumu mengine nje ya ofisi na kisha kuiahirisha kesi hii hadi Mei 17 na Mei, 18, 2023 ambapo itaendelea” amedai Kibatala.
Baada ya taarifa hivyo kutolewa na Kibatala, wanachama na wafuasi wa chama hicho walishuka chini kutoka ghorofa ya kwanza walipokuwa wamekaa wakisubiri kuingia mahakama ya wazi na kisha kuondoka katika viunga vya Mahakama hiyo.
Hata hivyo, taarifa nje ya mahakama zinaeleza kuwa kuna mkutano mkuu wa mwaka wa Majaji nchini nzima, unaoendelea jijini Mwanza.
Tayari Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Chadema, Dk Azaveli Lwaitama ameshahojiwa maswali ya dodoso na Wakili Ipilinga Panya anayewatetea Halima Mdee na wenzake.
Katika kesi hiyo Wabunge hao wanapinga uamuzi wa Baraza Kuu la Chadema wa Mei 11, 2022, kutupilia mbali rufaa zao za kupinga uamuzi wa Kamati Kuu wa Novemba 27, 2020 kuwafukuza uanachama kwa tuhuma za kuapishwa kuwa wabunge bila ridhaa ya Chama.
Leave a comment