KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, imeitaka Serikali kudhibiti uuzaji holela wa dawa za asili zisizopimwa ubora, ili kulinda afya za wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 2 Februari 2023 na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Stanslaus Nyongo, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu na shughuli za kamati kwa 2019/2020.
Akiwasilisha taarifa hiyo, Nyongo amesema kamati inaishauri Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu nchini (NIMR), kufanya utafiti dhidi ya dawa hizo ili kubaini ubora wake na kama ni salama kwa matumizi ya wananchi.
“Kupitia NIMR iweke mfumo wa kuhifadhi tafiti zote zinazofanyika nchini ili kujua na kutumia tafiti zote zinazofanyika kwa maslahi ya Taifa. Kuweka mpango mkakati wa kutenga fedha kutoka vyanzo vya ndani kwa ajili ya kufanya tafiti badala ya kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili wa nje ili kufanya tafiti nyingi zaidi,” amesema Nyongo akiwasilisha taarifa hiyo.
Aidha, Nyongo amesema, kamati hiyo ya Bunge inashauri NIMR iwekeze tafiti zaidi katika magonjwa yasiyoambukiza, kwa kuwa magonjwa hayo kwa sasa yanachangia asilimia kubwa zaidi ya vifo vya Watanzania.
Leave a comment