MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chadema, John Heche, ameonesha kushangazwa na matumizi ya Serikali yasiyo na tija huku ikiwaeleza wananchi kuwa hali ni mbaya kutokana na athari za Uviko-19 na vita vya Urusi na Ukraine. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, leo Alhamis tarehe 14 Julai, 2022, Heche amesema, “unaposema hali ni mbaya kwasababu ya Uviko, sijui vita ya Urusi, iathiri kuanzia mwananchi wa kawaida hadi Rais pale Ikulu.”
Mbunge huyo wa zamani wa Tarime Vijijini amesema licha ya kwamba ziara za Rais nje ya nchi ni muhimu lakini “isiwe kila siku.”
Amesema kwa nchi kama Tanzania ambayo ni masikini kiongozi kusafiri na timu ya zaidi ya watu 20 ni kuwatesa wananchi ambao ndio walipa kodi.
Amefafanua kuwa kipindi cha awamu ya Tano Chadema ilipinga Rais John Magufuli kutosafiri kabisa nje ya Afrika na kudai kuwa hawakumaani iwe kila siku.
“Wakati Magufuli hakusafiri kwenda nje na sisi tulisema sio sawa, Rais wa nchi lazima asafiri kwasababu Tanzania sio kisiwa lakini sio kila siku kiongozi anakwenda nje,” amesema Heche
Mbali na Rais, Heche amesema, “Waziri mzima anaweka mafuta kwenda kukagua anwani za makazi kule chini tuna watu wanaoweza kufanya hizo kazi kuna Mwenyekiti wa Mtaa.”
Amesema yupo Waziri mwingine (hajamtaja) “anasafiri kwenda kufundisha watu kuacha kutumia kuni na mkaa. Kuna mtu anapenda kutumia kuni na mkaa nchi hii? Amehoji Heche.
Amesema watu wanatumia kuni na mkaa kwasababu bei ya gesi “haishikiki, bei mtungi mmoja hadi Sh60,000.”
Amesema nchi kama Malawi wameweka bei ya umeme ni Sh10,000 kila mtu “upikie usipike bei ni 10,000 sasa nani ataenda kununua mkaa aache kutumia umeme?
Amesema endapo anataka wananchi wasitumie kuni na mkaa hana haja ya kwenda kuwafundisha, “unachotakiwa kufanya ni kuhakikisha kuna nishati ya uhakika ya kutumia inapatikana kwa bei nafuu.
“Hivi kweli Waziri unaweka mafuta, una msafara mnalipana posho, unaenda Tarime eti umekaa kwenye mafiga unafundisha mwananchi madhara ya kutumia kuni…kujua tu inasaidia nini, suluhu ni kuhakikisha wananchi wanakua wanapata nishati kwa gharama wanazozimudu,” amesema Heche.
Nakubaliana naye. Hii ni awamu ya vigogo kulamba asali na kula kwa kamba yao , ULAJI