HALI ya majonzi imetanda katika Chuo kikuu cha Laikipia nchini Kenya baada ya mwanafunzi mmoja wa kike kuuawa kinyama kwa kuchomwa kisu na jamaa anayedaiwa kuwa mpenzi wake. Anaripoti Glory Massamu, TUDARCo … (endelea).
Msichana huyo aliyefahamika kwa jina la Gertrude Chepkoech anadaiwa kuwa alikuwa akiishi katika chumba kimoja na mpenzi wake huyo aliyefahamika kwa jina la Ezra.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Kaunti ya Nyahururu, Marry Kiema amesema msichana huyo aliyekuwa na umri wa miaka 19, alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika chuo hicho akisomea kozi ya mawasiliano na kiingereza.
Kiema amesema msichana huyo alifariki kutokana na majeraha makubwa aliyopata kufuatia tukio hilo ambalo lilitokea muda wa alasiri jana tarehe 29 Septemba.
Amesema baada ya kutekeleza unyama huo, mshukiwa Ezra naye alitaka kujitoa uhai kwa kujichoma na kisu kwenye koo na tumboni.
Hata hivyo, Mmoja wa wafanyakazi katika hosteli ambayo marehemu alikuwa akiiishi, Lucy Nakaridi alisema kwamba mshukiwa alikuwa amesafiri kutoka Nakuru kuja kutembelea mpenzi wake ila mzozo ukatokea kati yao hadi ikalazimu uongozi wa hosteli na majirani kuingilia kati.
Nakaridi alisema kuwa msichana aliyekuwa ametembelewa alilalamika kwamba mshukiwa alikuwa analazimisha kutoka naye kimpenzi licha ya kumsisitiza waachane.
“Baada ya kufukuzwa inadaiwa kwamba jamaa hakuonekana pale tena hadi jana aliporudi na kuingia katika chumba cha mpenzi wake ambapo alimkuta akiwa peke yake.
“Muda mfupi baada ya Ezra kuingia kwenye hosteli zile majirani tulisikia mayowe makali kutoka kwenye chumba hicho na kukimbilia kuona kilichokuwa kinaendelea,” amesema Nakaridi.
Naye jirani mwingine aliyejitambulisha kama Reuben Rendile alisema kwamba walikuta mwili wa msichana ukiwa umelala sakafuni.
Rendille alisema kwamba mshukiwa alipowaona alijaribu kujitoa uhai kwa kujidunga kisu tumboni na kujikata koo.
“Majirani waliofika walimshambulia kwa kumpiga na fimbo kutokana na unyama alioutenda.
“Lakini polisi waliwahi kufika kwenye eneo la tukio wakamkamata mshukiwa na kumpeleka hospitali ya rufaa Nyahururu anakoendelea kupatiwa matibabu.
“Wakati mwili wa msichana huyo ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali hiyo,” amesema.
Leave a comment