CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemuonya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, asivuruge maandamano yao ya amani wanayofanya kupinga miswada ya marekebisho ya sheria za uchaguzi na kudai katiba mpya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza katika maeneo ya Buguruni Sheli, jijini Dar es Salaam, ambako maandamano hayo yanatarajiwa kuanza leo Jumatano, Naibu Katibu Mkuu Chadema Bara, Benson Kigaila, amedai wamepata taarifa kwamba Chalamila amefika maeneo hayo.
“Mkuu wa mkoa yupo hapa anaranda randa na magari wamepaki kule mbele akija hapa tutamfukuza, huo uhuni sisi hatuutaki. Mkuu wa mkoa asije hapa anataka kuvuruga maandamano yetu, ” amedai Kigaila.
Kigaila ametoa kauli hiyo wakati anawapa maelekezo wafuasi wa Chadema waliofika hapo kwa ajili ya kuandamana, ambapo amewataka wachukue tahadhari wakati wa tukio ikiwa pamoja na kufuata maelekezo ya viongozi wao.
Kigaila amewataka watu wote wanaofika maeneo hayo wasajiliwe ili idadi yao ijulikane.
Kuhusu bodaboda na magari yatakayokuwepo katika msafara huo, Kigaila amewataka wanaohusika nayo wafuate taratibu ili kukwepa usumbufu na madhara zaidi.
Amesema maandamano hayo ni ya amani kuelekea ofisi za Umoja wa Mataifa zilizoko maeneo ya Mlimani City jijini hapa.
Tayari askari polisi wako eneo la tukio wakiwa pembeni ya wafuasi wa Chadema.
Anayesubiriwa hadi muda huu wa saa 8.36 ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, awasili ili waanze maandamano hayo
Leave a comment