MUFTI na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dk. Sheikh Abubakar Zubeir bin Ali Mbwana ameitaka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni, (BRELA) kutoa elimu kwa umma ili waielewe na kufaidika na huduma inazozitoa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Sheikh Zubeir ametoa rai hiyo jana tarehe 3 Aprili 2024 katika hafla ya Iftar iliyoandaliwa na BRELA kwa wadau wake iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali na kufanyika Jijini Dar es Salaam.
Ameeleza kuwa, wapo watu waliofungua kampuni bila kufahamu jinsi ya kusimamia, BRELA iendelee kufungua milango ili watu wengi wapate kuifahamu taasisi na inachokifanya ili kuwasaidia kufanya biashara kwa mujibu wa sheria.
“Taasisi itoe elimu kuhusiana na masuala ya BRELA kwa kuwa wapo wengi huitaja Wakala lakini hawajui inafanya nini, hivyo ni muhimu kuwaelimisha ili watafahamu huduma zinazotolewa, jinsi ya kuzipata na umuhimu wake,”Alisema Sheikh Zubeir
Akieleza umuhimu wa elimu Sheikh Zubeir amefafanua kuwa mtu huweza kuharibikiwa na mambo mengi asipokuwa na elimu huku akitanabaisha kuwa ujinga ni aibu na hakuna anayeukubali na akauridhia.
Katika hatua nyingine Sheikh Zubeir amempongeza Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa kwa kuandaa iftar kwa mara ya kwanza na kushukuru kwa kumwalika pamoja na wadau wengine kuwa watu wa kwanza kushiriki katika tukio hilo, na kumsihi kuwa zoezi hilo liwe endelevu.
“Awali nilimuuliza Nyaisa hii ni Iftar ya ngapi kufanya, akanieleza kuwa hii ndio mara ya kwanza zoezi kama hili linafanyika, nampogeza sana kwa kuandaa n ani Imani yangu kwamba mtaendelea kufanya vizuri zaidi,” amesema Sheikh Zubeir.
Awali akimkaribisha Mufti katika hafla hiyo, Nyaisa, alimshukuru Mufti na Sheikh Mkuu kwa kukubali kushiriki katika hafla ya Iftar ya kwanza kwa BRELA na kuahidi kuboresha zaidi sambamba na kuwakumbuka watu wenye uhitaji.
BRELA imeandaa iftar hiyo kwa mara ya kwanza kwa lengo la kuwa karibu na wadau ambapo Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dk. Sheikh Abubakar Zubeir bin Ali Mbwana alikuwa mgeni rasmi wa hafla hiyo.
Leave a comment