JOTO la chaguzi linapanda kila siku hapa nchini. Upo umuhimu wa wanasiasa na viongozi wa dini kujiepusha na uchonganishi, uchokozi na kufuru.
- Kusema Rais wetu anaupendelea mkoa fulani kuliko mingine ni uchonganishi. Rais wetu anaipenda mikoa yote kwa usawa na aliapa hadharani kufanya hivyo.
- Rais wetu hajateua mtoto wake katika nafasi yoyote ya utumishi wa umma. Ikitokea, atakuwa amemteua kama mtu mwingine yeyote, si kama mtoto wake. Huu ni uchokozi.
- Kuna tofauti kati ya mtoto wa pekee na Mwana wa pekee. Rais wetu hana Mwana wa Pekee kwa sababu siyo Mungu na Rais wetu hana mtoto wa pekee kwa sababu aliishatutangazia na tunawajua watoto wake. Kusema Rais ametuma Mwana wa pekee ni kufuru. Kusema Rais wetu ana mtoto wa pekee ni uchokozi pia.
- Kusema “sitajali Baba yako ni nani” ni sahihi, na inatakiwa iwe hivyo. Lakini kusema “sitajali ulipata nafasi hiyo kwa kuhonga, rushwa au kwa waganga” lina ukakasi wa hatari. Ni zaidi ya kuchonganisha, kuchokoza na kubagaza. Kumbe hao wapo pia?
- Kitendo cha watu kutaka kuwaua au kuwadhuru viongozi wetu wa umma ni tishio la usalama wa nchi. Tusikubali kulea tatizo hili. Viongozi wetu wasiishie kutuhumu bila kuchukua hatua. Inaleta taharuki katika jamii kusikia kiongozi wetu amenusurika mara tatu kuuawa na hakuna waliokamatwa au kutajwa hadharani. Ni ama viongozi wasiseme kabisa hadharani au wahusika watajwe na kuchukuliwa hatua.
- Viongozi wa kisiasa, wa kidini na wa kijamii, natamani mtambue kuwa kipaza sauti kinaua kuliko sumu. Mungu atujalie kujisikiliza kabla ya kusikilizwa. Hata mimi ninatamani ningekaa kimya ili hili lipite. Nimeshindwa. Mnisamehe. Siwezi kuahidi kuwa sitarudia.Kwa Mungu wangu na Taifa langu. Makala hii imeandaliwa na Askofu Benson Bagonza.
Leave a comment